Na CECIL ODONGO
KOCHA wa Nzoia Sugar Salim Babu amesema kuwa hawatabanduka kileleni mwa msimamo wa jedwali kwa kuwa msimu huu lengo lao ni kutwaa taji la Ligi Kuu (KPL).
Nzoia ilishinda ligi mara ya mwisho mnamo 2001 na msimu huu wamekuwa moto wa kuotea mbali kwa kuwachapa wapinzani kiholela.
Kinyume na misimu iliyopita ambapo timu hiyo ilikuwa ikinusurika pembemba kushushwa ngazi, mara hii wao ni moto wa kuotea mbali wakiongoza msimamo wa jedwali kwa alama 21 kutokana na mechi 10.
Kenya Commercial Bank (KCB) pia ina alama 21 baada ya mechi 10 na inashikilia nafasi ya pili japo inadunishwa na uchache wa mabao ikilinganishwa na Nzoia Sugar.
Wanasukari hao wana wachezaji wachanga wenye umri wa wastani wa miaka 21 ambao wana kasi ya kutisha.
Mabingwa watetezi Tusker nao wanaendelea kuona vumulimuli baada ya kushindwa kupata alama tatu katika mechi tatu mfululizo na sasa wameshuka hadi nafasi ya tatu kwa alama 20.
“Sisi hatushikilii timu nyingine nafasi ya juu kwa kuwa lengo letu ni kushinda mechi zetu na kutwaa KPL. Tumetulia vizuri na wenye dukuduku watangoja sana kwa sababu bado tutawika. Tuna wanasoka wenye nidhamu na wanaofikiria vinginevyo watashangaa,” akasema Babu, 37 ambaye alikuwa mkufunzi wa Wazito na SoNy Sugar.
Wakataji miwa hao wamemiminiwa sifa kedekede kutokana na mtindo wao wa kucheza mpira ambao mpira hubusu nyasi na wachezaji huonana vyema kabla ya kufunga goli.
Mnamo Jumatano, Nzoia ilipiga pasi 15 fupifupi kuelekea goli lao la tatu kwenye ushindi wa 4-0 dhidi ya Wazito. Msimu huu hakuna timu yoyote ambayo imetoka na alama tatu katika uga wao wa nyumbani wa Sudi.
Pia Nzoia Sugar imedondosha alama mara tatu pekee baada ya kuchapwa na Gor 1-0 mnamo Novemba 19 kisha ikaenda sare tasa dhidi ya Bandari na Tusker mnamo Novemba 26 na Januari 14.
Tusker ndiyo bado timu ambayo imefunga mabao mengi KPL baada ya kucheka na nyavu za wapinzani mara 15 huku ikifuatwa na Ulinzi kwa alama 14.
Kocha wa Gor Mahia Johnathan McKinstry huenda naye akajipata pabaya mikononi mwa mashabiki baada ya sare tasa dhidi ya Sofapaka.
Mashabiki walimkemea kocha huyo kutokana na mbinu zake zisizoridhisha za ukufunzi baada ya sare dhidi ya Sofapaka.
Subscribe our newsletter to stay updated