• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 7:53 PM
Olunga pua na mdomo kuyoyomea Qatar kuvalia jezi za Al-Duhail SC

Olunga pua na mdomo kuyoyomea Qatar kuvalia jezi za Al-Duhail SC

Na CHRIS ADUNGO

KASHIWA Reysol ambao ni waajiri wa fowadi Michael Olunga wa Harambee Stars wako radhi kukubali ofa ya Sh940 milioni kwa minajili ya kufanikisha uhamisho wa nyota huyo hadi kambini mwa Al-Duhail SC ya Qatar.

Mabingwa hao mara saba wa Ligi Kuu ya Qatar wanatarajiwa kuanza mazungumzo na Olunga, 26, wiki hii kwa matarajio kwamba atawasaidia kutia kapuni taji lao la nane ligini.

Chini ya mkufunzi Sabri Lamouchi, Al-Duhail kwa sasa wanajivunia pia huduma za beki matata wa zamani wa Juventus Medhi Amine El Mouttaqi Benatia anayeshirikiana na vilivyo na nyota raia wa Tunisia, Youssef Msakni.

Olunga ambaye kwa sasa hutia mfukoni ujira wa takriban Sh8 milioni kwa mwezi, anahusishwa pia na vikosi kadhaa vya Ligi Kuu ya Italia, Ufaransa na Uturuki.

Mwishoni mwa mwaka wa 2020, Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) lilimtia Olunga katika orodha ya wanasoka watano wa haiba kubwa ambao hawajulikani sana licha ya kuwika mno katika kampeni za mwaka wa 2020.

“Japo nimepokea ofa nyingi za kujiunga na vikosi mbalimbali vya bara Ulaya, lengo langu ni kusalia nchini Japan kwa matumaini ya kuendelea kufungiwa Kashiwa mabao mengi zaidi. Hata hivyo, wakala wangu atakuwa huru kutathmini hali ilivyo kabla ya kushauriana nami kuhusu maamuzi mengine muhimu kitaaluma,” akatanguliza Olunga.

“Iwapo nitalazimika kuondoka Japan, basi itamaanisha kwamba ofa mpya nitakayokuwa nimepata ni ya kuridhisha zaidi kiasi kwamba ni vigumu kabisa kuipuuza,” akaongeza fowadi huyo.

Olunga aliwahi pia kufichua ukubwa wa kiu ya kuingia katika sajili rasmi ya Arsenal ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) chini ya kocha wa zamani wa kikosi hicho, Arsene Wenger.

Nyota huyo wa zamani wa Gor Mahia alijivunia msimu wa kuridhisha katika Ligi Kuu ya Japan (J1 League) na akatawazwa Mchezaji Bora na Mfungaji Bora muhula huu baada ya kucheka na nyavu mara 28 kutokana na mechi 32.

Katika mechi yake ya msimu huu ndani ya jezi za Reysol, Olunga alifunga bao japo wakapokezwa kichapo cha 2-1 kutoka kwa FC Tokyo kwenye fainali ya kuwania ubingwa wa taji la Levain Cup mnamo Januari 4, 2021.

Makali ya Olunga mbele ya malango ya wapinzani yalisaidia waajiri wake Reysol kukamilisha kampeni za msimu huu za Ligi Kuu ya Japan katika nafasi ya saba jedwalini licha ya kwamba walipandishwa ngazi mwishoni mwa muhula uliopita ulioshuhudia sogora huyo wa zamani wa Gor Mahia akifunga mabao 27.

Japo Olunga amewahi pia kuchezea nchini Uswidi, Uhispania na China, wepesi wake wa kufunga mabao umejitokeza katika kipindi cha misimu miwili iliyopita nchini Japan.

“Mafanikio yangu ulingoni ni zao la imani na bidii. Sikuwahi kutamauka hata nilipojikuta nikikabiliwa na changamoto tele. Natambua pia ukubwa wa mchango wa wanasoka wenzangu ambao waliniundia pasi nyingi zilizozalisha idadi kubwa ya mabao niliyofunga,” akasema Olunga katika mahojiano yake na Fifa.com.

Kati ya rekodi nyinginezo zinazojivuniwa na Olunga katika ulingo wa soka ni kuwahi kuwa sogora wa kwanza kufungia FC Girona ya Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) jumla ya mabao matatu katika mechi moja ligini.

Mchezaji huyo wa zamani wa Liberty Sports Academy, Tusker FC na Thika United aliwahi pia kufungia Kashiwa jumla ya mabao manane katika ushindi wa 13-1 uliosajiliwa na kikosi hicho dhidi ya Kyoto Sanga katika Ligi ya Daraja la Pili mnamo 2019.

Kabla ya kujiunga na Girona kwa mkopo kutoka Guizhou Zhicheng ya China iliyomuuza kwa Sh56 milioni, Olunga aliwahi pia kusakata soka ya kulipwa kambini mwa Djurgardens IF ya Uswidi mnamo 2016.

Nyota huyo amekuwa tegemeo kubwa la timu ya taifa ya Harambee Stars na mabao yake dhidi ya Ghana na Ethiopia yalisaidia Kenya kufuzu kwa fainali za Kombe la Afrika (AFCON) mnamo 2019 nchini Misri.

Olunga alifungia Stars mabao matatu kwenye fainali hizo zilizoshuhudia Kenya ikibanduliwa mapema kwenye Kundi C lililojumuisha pia Tanzania, Senegal na Algeria.

You can share this post!

COVID-19: Walimu kuwa miongoni mwa watu wa mwanzo...

Spurs wakomoa Brentford 2-0 na kufuzu kwa fainali ya...