• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Pigo kwa Man-City beki tegemeo Ruben Dias akitarajiwa kusalia mkekani kwa wiki sita zijazo

Pigo kwa Man-City beki tegemeo Ruben Dias akitarajiwa kusalia mkekani kwa wiki sita zijazo

Na MASHIRIKA

BEKI matata wa Manchester City na timu ya taifa ya Ureno, Ruben Dias, 24, sasa atasalia nje kwa takriban wiki sita kutokana na jeraha la paja.

Hadi kufikia sasa, Dias amekosa mechi tatu pekee kutokana na 28 ambazo zimetandazwa na waajiri wake katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

“Ni mchezaji muhimu ambaye tukakosa huduma zake. Upekee wa mchango wake ni miongoni mwa sababu ambazo zimetudumisha kileleni mwa jedwali la EPL kwa kipindi kirefu,” akasema kocha Pep Guardiola.

Dias sasa anatarajiwa kukosa mechi tano zijazo za Man-City ambao wameratibiwa kumenyana na Sporting, Crystal Palace, Southampton, Burnley na Liverpool kwa usanjari huo.

Ingawa Man-City wanajivunia pengo la alama sita kuliko nambari mbili Liverpool kileleni mwa jedwali la EPL, mabingwa hao watetezi wametandaza mechi moja zaidi kuliko 27 ambazo zimepigwa na Liverpool.

Dias aliingia rasmi katika sajili ya Man-City baada ya kuagana na Benfica ya Ureno kwa Sh9.8 bilioni mnamo Septemba 2020. Tangu wakati huo, amesaidia Man-City kukamilisha mechi 26 kati ya 57 bila kufungwa na akaongoza waajiri wake hao kunyanyua taji la EPL na Carabao Cup mnamo 2020-21.

Man-City wataalika Sporting Lisbon ya Ureno katika mkondo wa pili wa hatua ya 16-bora ya UEFA mnamo Machi 9, 2022 ugani Etihad kabla ya kuendea Palace ya kocha Patrick Vieira katika EPL siku tano baadaye ugani Selhurt Park.

Baada ya hapo, miamba hao watamenyana na Southampton katika robo-fainali za Kombe la FA mnamo Machi 19, 2022 kabla ya kurejelea kampeni za EPL dhidi ya Burnley, Liverpool, Wolves na Watford kwa usanjari huo.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Hila ya Uhuru kuwa na nguvu akistaafu

Chuma chenu ki motoni, PCPB yaambia wauzaji wa dawa feki za...

T L