• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 6:40 PM
Poland yapepeta Uswidi na kujikatia tiketi ya kuelekea Qatar kwa Kombe la Dunia

Poland yapepeta Uswidi na kujikatia tiketi ya kuelekea Qatar kwa Kombe la Dunia

Na MASHIRIKA

POLAND walifuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2022 nchini Qatar baada ya mabao kutoka kwa Robert Lewandowski na Piotr Zielinski kuzamisha Uswidi 2-0 katika fainali ya mchujo mnamo Jumanne usiku.

Lewandowski aliwaweka Poland kifua mbele kupitia penalti ya dakika ya 49 baada ya Grzegorz Krychowiak kuchezewa visivyo ndani ya kijisanduku. Zielinski alichuma nafuu kutokana na masihara ya mabeki wa Uswidi na kufungia Poland bao la pili katika dakika ya 72.

Poland sasa watasubiri kufahamu vikosi watakavyokutana navyo katika hatua ya makundi baada ya droo ya fainali za Kombe la Dunia kufanyika Ijumaa ya Aprili 1, 2022. Fainali zijazo za Kombe la Dunia zitafanyika Qatar kati ya Novemba na Disemba 2022.

Kigogo Zlatan Ibrahimovic aliletwa ugani na timu ya taifa ya Uswidi katika dakika ya 80. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 40 anayechezea AC Milan sasa ametandaza mchuano wake wa mwisho katika safari ya kuongoza Uswidi kufuzu kwa Kombe la Dunia. Uswidi waliokomoa Jamhuri ya Czech 1-0 kwenye nusu-fainali mnamo Machi 24, 2022, walishuka ugani Slaski kuvaana na wenyeji Poland wanaojivunia maarifa ya mvamizi Lewandowski na kipa Wojciech Szczesny.

Poland walitinga fainali baada ya Urusi waliokuwa wavaane nao kwenye nusu-fainali kupigwa marufuku na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) kwa sababu ya uvamizi wao dhidi ya Ukraine. Hadi walipotandikwa na Poland, Uswidi walikuwa wameangusha Poland katika mechi sita za awali mfululizo, ushindi wa karibuni zaidi ukiwa 3-2 katika makundi ya fainali za Euro 2020.

You can share this post!

Timu ya ufukweni leo itafahamu kama itashiriki Madola

Bruno Fernandes abeba Ureno hadi fainali za Kombe la Dunia...

T L