• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 6:50 AM
Raga: Vidume wa Shamas RFC bado juu ligi ya kitaifa

Raga: Vidume wa Shamas RFC bado juu ligi ya kitaifa

Na TITUS MAERO

LICHA ya kikosi cha Shamas Foundation RFC kushindwa kwenye mechi ya raundi ya tatu ya Ligi ya Kitaifa Daraja ya Kwanza (Championship) wikendi iliyopita, bado kimesalia kileleni mwa jedwali la kipute hicho cha Shirikisho la Raga Nchini (KRU) .

Timu hiyo iko juu ya msimamo kwa alama 11 baada ya kulishwa kichapo cha 8-5 kutoka kwa Chuo Kikuu cha Kabarak, katika uwanja wa chuo hicho mnamo Jumamosi.Shamas Foundation na Kabarak zilipandishwa ngazi kutoka Daraja ya Pili (Nationwide) baada ya kutinga fainali ya kinyang’anyiro hicho msimu uliopita.

Mshindi wa Championship mwishoni mwa msimu huu atajikatia tiketi ya moja kwa moja kujiunga na Ligi Kuu ya Raga (Kenya Cup) msimu ujao. Hapo jana, nahodha Simon Sechere wa Shamas aliambia Taifa Spoti mjini Kakamega kuwa, wanalenga kujinyanyua na kufana katika mechi zijazo.

“Azma yetu ni kujiunga na Ligi Kuu msimu ujao,” Sechere alieleza huku ligi hiyo ikienda likizoni hadi Januari. Nambari mbili katika jedwali Mean Machine RFC ya Chuo Kikuu cha Nairobi (UoN), walijiongezea alama hadi pointi 10 baada ya kucharaza Eldoret RFC 43-7 jijini Nairobi.

Timu ya Chuo Kikuu cha Catholic, almaarufu Catholic Monks RFC, iliteremka hadi nafasi ya tatu baada ya kupepetwa 29-17 na Western Bulls RFC mjini Kakamega. Monks sasa wana alama 10 katika msimamo wa ligi.“Masogora wangu walionyesha mchezo wa hali ya juu.

Ni matumaini yangu kwamba wataendelea kufanya hivyo,” kocha Sabastian Obiero wa Western Bulls aliambia Taifa Spoti mjini Kakamega jana. South Coast Pirates RFC wanakamata nambari nne ligini wakiwa na pointi nane.Eldoret RFC nayo inashikilia nafasi ya tano pia kwa alama nane ila kwa uchache wa pointi za bonasi.

Kikosi cha Western Bulls RFC kiko katika nafasi ya sita kwa pointi saba.Chuo Kikuu cha Eldoret (UoE) pia wako na alama saba ila kwa uchache wa pointi za bonasi. Wanachuo wa USIU-A wamejizolea alama sita , Kabarak wako na pointi nne nao Northern Suburbs RFC wako na tatu.

Timu ya Chuo Kikuu cha Egerton, almaarufu Egerton Wasps RFC, na Kisumu RFC bado hazifanikiwa kupata pointi yoyote ligini msimu huu.

You can share this post!

Kizaazaa EFL Cup leo soka ikisonga mbele

Tusker kuvaana na Homeboyz, Gor vs Posta ikiahirishwa

T L