Na MASHIRIKA
REAL Madrid walinyimwa fursa ya kushinda mechi ya nane mfululizo katika Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) baada ya kulazimishiwa sare tasa na wanyonge Cadiz uwanjani Santiago Bernabeu mnamo Jumapili.
Matokeo hayo hata hivyo bado yalisaza Real kileleni mwa jedwali la La Liga kwa alama 43, sita zaidi kuliko nambari mbili Sevilla ambao wana mechi moja zaidi ya kutandaza ili kufikia idadi ya michuano ambayo tayari imepigwa na Real.
Chini ya kocha Carlo Ancelotti, Real walitamalaki mchezo na wakaelekezea Cadiz makombora 36. Miamba hao walipoteza nafasi nyingi za kufunga mabao kupitia kwa Eden Hazatd, Karim Benzema na Vinicius Jr aliyekuwa akinogesha mchuano wake wa 100 katika La Liga. Hazard alikuwa akiwajibishwa ligini kwa mara ya kwanza tangu katikati ya Septemba 2021.
Nusura Alvaro Negredo afungie Cadiz bao muhimu mwishoni mwa kipindi cha pili. Cadiz sasa wanakamata nafasi ya 19 jedwalini kwa pointi 14, sita mbele ya Levante wanaovuta mkia.
MATOKEO YA LA LIGA (Jumapili):
Real Madrid 0-0 Cadiz
Granada 4-1 Mallorca
Bilbao 3-2 Real Betis
Getafe 1-0 Osasuna