Na MASHIRIKA
MATUMAINI ya Paris Saint-Germain (PSG) kutia kapuni taji la Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1) msimu huu yalididimia zaidi Jumapili baada ya Rennes kuwalazimishia sare ya 1-1.
Neymar aliwaweka PSG kifua mbele mwishoni mwa kipindi cha kwanza kupitia penalti iliyotokana na tukio la beki raia wa Ufaransa, Layvin Kurzawa kuchezewa visivyo ndani ya kijisanduku.
Hata hivyo, Serhou Guirassy alisawazishia Rennes kunako dakika ya 70, muda mfupi kabla ya difenda Presnel Kimpembe wa PSG kuonyeshwa kadi nyekundu.
Sare iliyosajiliwa na masogora wa kocha Mauricio Pochettino dhidi ya Rennes iliwadumisha PSG katika nafasi ya pili jedwalini kwa alama 76, tatu zaidi nyuma ya viongozi Lille. Zimesalia mechi mbili pekee kwa kampeni za Ligue 1 msimu huu kutamatika rasmi.
Matokeo hayo yaliendeleza masaibu ya Pochettino aliyeshuhudia kikosi chake kikidenguliwa na Manchester City kwenye nusu-fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Mei 4, 2021.
MATOKEO YA LIGUE 1 (Mei 9, 2021):
Rennes 1-1 PSG
St-Etienne 1-0 Marseille
Angers 3-0 Dijon
Metz 0-3 Nimes
Nice 3-2 Brest
Strasbourg 2-3 Montpellier
Reims 0-1 Monaco