• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Richarlson aongoza Brazil kupepeta Ghana katika mechi ya kujinoa kwa fainali za Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar

Richarlson aongoza Brazil kupepeta Ghana katika mechi ya kujinoa kwa fainali za Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar

Na MASHIRIKA

FOWADI mpya wa Tottenham Hotspur, Richarlson Andrade, alifunga mabao mawili katika kipindi cha kwanza na kusalia Brazil kupepeta Ghana 3-0 katika pambano la kirafiki mnamo Ijumaa.

Richarlson, 25, alishirikiana vilivyo na Neymar katika safu ya mbele baada ya wavamizi wawili wa Arsenal – Gabriel Jesus na Gabriel Martinelli – kutojumuishwa katika kikosi cha Brazil.

Beki mzoefu wa Paris St-Germain (PSG), Marquinhos, aliwaweka Brazil kifua mbele kunako dakika ya tisa baada ya kukamilisha krosi aliyomegewa na Raphinha.

Brazil walipanga kikosi chao thabiti katika pambano hilo lililonogeshwa pia na kipa wa Liverpool, Allison Becker, beki Thiago Silva wa Chelsea, kiungo Carlos Casemiro wa Manchester United na kiungo mahiri wa Liverpool, Fabinho Tavares.

Chini ya kocha Adenor Tite, Brazil kwa sasa watavaana na Tunisia katika pambano jingine la kirafiki mnamo Septemba 27, 2022. Mechi hiyo itakuwa sehemu ya maandalizi ya fainali za Kombe la Dunia nchini Qatar ambapo wamepangiwa kupepetana na Serbia, Uswisi na Cameroon katika kundi lao. Brazil watakuwa wakiwania ufalme wa dunia kwa mara ya sita nchini Qatar.

Kwingineko, nyota wa Liverpool, Mohamed Salah, alifunga mabao mawili ikiwemo penalti, na kusaidia timu yake ya taifa ya Misri kutandika Niger 3-0 kirafiki mnamo Ijumaa. Misri hawakufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2022 nchini Qatar.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

GASPO Women ya KWPL yasajili 10

Kiungo wa Brazil, Allan, aondoka Everton na kuyoyomea UAE...

T L