Na GEOFFREY ANENE
Orodha ya watimkaji wa mbio za kilomita 42 kutoka Kenya watakaoshiriki mbio za kifahari za Berlin Marathon hapo Septemba 26 imetangazwa Septemba 2.
Mabingwa Purity Rionoripo (Paris Marathon), Ruth Chebitok (Gold Coast Marathon) na Eliud Kiptanui (Prague Marathon) ni baadhi ya majina makubwa kutoka Kenya watakaowania tuzo ya mshindi ya Sh5.2 milioni.
Pia, kuna Edith Chelimo, Philemon Kacheran, Festus Talam, Michael Njenga na Benard Kimeli.
Mabingwa watetezi ni Waethiopia Kenenisa Bekele (wanaume) na Ashete Bekere (wanawake). Bekele, ambaye alikosa rekodi ya dunia ya Mkenya Eliud Kipchoge kwa sekunde mbili akitwaa taji la 2019 kwa saa 2:01:41, atakuwa uwanjani kutetea ubingwa wake.
Watimkaji wengine wanatoka mataifa ya Ethiopia, Ujerumani, Poland, Mongolia, Uswizi, Israel, Japan na Eritrea. Bonasi ya kuweka rekodi mpya Berlin ni Sh6.5 milioni. Rekodi nane za dunia zimewahi kuwekwa jijini Berlin ikiwemo ya wanaume ya 2:01:39 inayoshikiliwa na bingwa wa Olimpiki Kipchoge tangu 2018.