• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Salah apongeza Harambee Stars na kupatia Muguna jezi

Salah apongeza Harambee Stars na kupatia Muguna jezi

Na GEOFFREY ANENE

VIDEO ya nyota Mohamed Salah akipongeza Harambee Stars katika chumba cha kubadilishia mavazi baada ya Harambee Stars kutoka nyuma na kukaba Misri 1-1 Alhamisi, imetokea.

Mvamizi huyo matata wa Liverpool alinyamzishwa uwanjani Kasarani katika mechi hiyo ya Kundi G ya kufuzu kushiriki Kombe la Afrika (AFCON) 2022 ambayo hata hivyo Misri ilipata alama moja iliyohitaji ya kujikatia tiketi, huku Kenya ikibanduliwa.

Salah hakuwa na mechi nzuri ugani humo, pengine akihofia kupata jeraha, na alipata ugumu kupenya safu ya ulinzi ya vijana hao wa kocha Jacob ‘Ghost’ Mulee, akionekana kuzidiwa kasi, nguvu na pia fomu.

Hata hivyo, alipata umaarufu zaidi nje ya uwanja baada ya video kutokea akiwa katika chumba cha kubadilishia mavazi cha timu ya Kenya mechi hiyo ilipokatika akiwapongeza kwa kuonyesha mchezo mzuri. Pia, aliwatakia kila la kheri katika majukumu mengine yaliyo mbele yao baada ya kushindwa kufika AFCON2022.

Katika chumba hicho pia kulikuwa na benchi ya kiufundi pamoja na rais wa Shirikisho la Soka Kenya (FKF) Nick Mwendwa.

Isitoshe, Salah pia alipatia jezi yake kiungo wa Gor Mahia Kenneth Muguna ambaye alikuwa na mchezo wa kupendeza dakika zote 90. Video hiyo iliyowekwa kwenye mitandao ya kijamii imepata kutazamwa na maelfu ya watu na pia kuchapishwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).

  • Tags

You can share this post!

Lewandowski awazolea Poland alama moja muhimu dhidi ya...

Ibada yaendelea Chato kabla ya Magufuli kuzikwa baadaye leo