• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 5:55 AM
Samwest Black Boots yajipatia miaka minne kutinga ligi kuu

Samwest Black Boots yajipatia miaka minne kutinga ligi kuu

Na JOHN KIMWERE

TIMU ya Sam West Black Boots FC ni kati ya vikosi vinavyopania kupambana mwanzo mwisho kuhakikisha vimetwaa ubingwa wa kipute cha Central Regional League (CRL) muhula huu. Kikosi hicho kiliobadilisha jina mwishoni mwa mwaka jana awali kilifahamika kama Gachui Black Boots.

”Tulibadilisha jina baada ya mfanyi biashara wa maduka ya Sam West Distributors jijini Nairobi, Samuel Njuguna Kimani kutangaza kuwa atakuwa mfadhili wetu kwenye jitihada za kukuza wanasoka wenye kipaji cha mchezo huo,” ofisa mkuu wake, Isaac Mwaura anasema na kuongeza kuwa wana imani tosha kuwa ufadhili huo utawatia motisha zaidi wachezaji hao na kufanya kweli kwenye kampeni za ngarambe hiyo muhula huu.

Anadokeza kuwa kabla ya mfanyi biashara huyo kutangaza kuwa mfadhili wao alianza kuwashika mkono mwishoni mwa mwaka uliyopita. Mfanyi biashara huyo atakuwa mdhamini mkuu ambapo ametangaza kugharamia mahitaji yote ikiwamo kulipa wachezaji hao marupurupu, kuwalipia bima ya afya pia amewapa gari aina ya basi watakayotumia kusafirisha wachezjai hao kushiriki mechi zote za ligi.

”Bila shaka tunamshukuru zaidi mfanyi biashara huyo kwa hatua aliyochukua kufadhili timu yetu iliyoasisiwa mwaka 1995 na hupatikana eneo la Gachui Kaunti ya Nairobi,” akasema. Ofisa huyo anafichua kuwa mfadhili huyo analenga kusaidia klabu hiyo hadi itimiza azimio lake kufuzu kupandishwa ngazi kushiriki kinyang’anyiro cha FKF-PL.

Kadhalika ofisa huyo anashikilia kuwa wamepania kukaza buti kuhakikisha ndani ya miaka minne watafuzu kupandishwa daraja kushiriki mechi za kipute cha haiba kubwa nchini. Baada ya mfanyi biashara huyo kutangaza ufadhili huo klabu hiyo ilitwaa huduma za kocha mpya, Christopher Wekesa aliyekuwa mchezaji wa kimataifa na Harambee Stars.

Timu ya Sam West Black Boots iliyokuwa ikifahamika kama Gachui Black Boots FC…Picha/JOHN KIMWERE

”Ninaamini nina tajiriba tosha kubeba timu yangu mpya kuifikisha kiwango cha kutosha mboga kushiriki ligi ya hadhi ya juu nchini,” kocha huyo alisema na kuongeza kuwa wanafanya vizuri kwenye mechi za ligi hali inayowatia motisha zaidi kwenye kampeni za muhula huu. Anatahadhirisha wapinzani wao kuwa kamwe hawapo tayari kudondosha mchezo wowote kwenye kampeni za kipute hicho.

Kadhalika anasema kuwa ana imani wachezaji wanne waliosajili kabla ya mwanzo wa ligi muhula huu watachochea wenzao kwenye kampeni za kipute hicho. Kufikia sasa SamWest Black Boots chini ya nahodha, Bonface Wainaina ambayo imepangwa Kundi C kwenye mechi za CRL inaongoza kwa kuzoa alama tisa baada ya kushiriki mechi tatu. Destiny FC inashikilia nafasi ya pili kwa alama saba sawa na Gikambura Homebyz FC.

Wekesa ana historia pevu kwa kuzingatia kando na timu ya taifa pia alichezea Hope Centre ambayo ndio City Stars maarufu kama Simba wa Nairobi. Aidha alisakatia Yassets FC, Kawangware United, Gor Mahia pia alishiriki soka la kulipwa nchini Ethiopia na Singapore. Wekesa anajivunia kunoa makucha ya wachezaji wa Nakumatt FC, Mt Kenya na Compassion FC.

Sam West Black Boots inajumuisha:Michael Kibiru (naibu nahodha), Moses Lidonde, Frederick Owino, Emmanuel Ngaira, Kenneth Ndungi, Mastron Okoth, Martin Karanja, Arcadious Karanja, Francis Muongi, Dairus Ndungi, Alex Manyara na Christopher Otieno. Pia wapo Shadrack Gichuhi, Bonface Wainaina, Simon Kimani, Dennis Njogu, Frederick Ngigi, William Ochieng, Kevin Njuguna, Patrick Mwangi. Martin Kibinu, George Ndungu, Joshua Ondieki na Bernard Kimani. Sam West Black Boots ilibanduliwa katika hatua za robo fainali kwenye kampeni za kipute cha Dagoretti Cup muhula huu.

Kocha Christopher Wekesa. …Picha/JOHN KIMWERE

You can share this post!

Isiolo Young Stars yapania kulea wengi kuchezea timu za...

Serikali yajitolea kuendelea kukabiliana vilivyo na...

T L