• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Shujaa wazidiwa maarifa Hamilton 7s kujiweka pabaya zaidi Raga za Dunia

Shujaa wazidiwa maarifa Hamilton 7s kujiweka pabaya zaidi Raga za Dunia

Na GEOFFREY ANENE

KENYA Shujaa hawakuwa na lao katika Kundi A baada ya kuzidiwa maarifa na Samoa, Fiji na Ufaransa kwenye duru ya nne ya Raga za Dunia mjini Hamilton, New Zealand, mapema Jumamosi.

Vijana wa kocha Damian McGrath walifungua kampeni vibaya walipochapwa 31-5 katika mechi ambayo Anthony Omondi alipachika mguso wa kufutia machozi.

Mabingwa wa Cape Town Sevens – Samoa – walitangulia kuona lango kupitia kwa Owen Niue dakika ya tatu.

Omondi alisawazisha dakika nne baadaye na kuenda mapumzikoni bega kwa bega 5-5.

Hata hivyo, Kenya iliona vimulimuli katika kipindi cha pili ilipoongezwa miguso minne bila jibu na mikwaju mitatu.

Katika mchuano wa pili dhidi ya Fiji, Brian Tanga alifungia Shujaa mguso wa kujiondolea aibu ulioandamana na mkwaju kutoka kwa Dennis Abukuse.

Wanavisiwa wa Fiji walitawala 21-7. Vijana wa McGrath walitoa Ufaransa kijasho katika mchuano wa mwisho wa makundi, ingawa waliishia kuupoteza 26-21.

Shujaa ilijipata chini 14-0 Nelson Epee alipotinga miguso miwili iliyoandamana na mikwaju kutoka kwa Paulin Riva. Ilisawazisha 14-14 kupitia miguso ya Omondi na Alvin ‘Buffa’ Otieno.

Omondi aliongeza mikwaju ya miguso hiyo. Epee aliingiza Ufaransa mapumzikoni kifua mbele 19-14 alipoongeza mguso. Wafaransa waliimarisha uongozi hadi 26-14 kupitia mguso na mkwaju kutoka kwa Riva.

Kenya ilihitimisha mchuano huo kwa kupata mguso kutoka kwa Tanga na mkwaju kupitia kwa Omondi. Shujaa iliratibiwa kuvaana na Canada Jumamosi usiku kwenye robo-fainali ya kuorodheshwa nambari tisa hadi 16.

  • Tags

You can share this post!

Kamusinga yaongoza Magharibi

DINI: Utavuna ulichopanda, hakuna mkato maishani!

T L