Na GEOFFREY ANENE
TIMU ya taifa ya raga ya wachezaji saba kila upande ya Kenya maarufu kama Shujaa inaingia kambi ya mazoezi ya timu ya Olimpiki ya Kenya uwanjani Kasarani hii leo.
Kocha mkuu Innocent “Namcos” Simiyu ameeleza Taifa Leo kuwa vijana wake wataelekea nchini Afrika Kusini kushiriki shindano la mwaliko mnamo Mei 8-9.
“Wachezaji na maafisa wa timu ya Shujaa wote walipokea chanjo dhidi ya corona ya AstraZeneca,” Simiyu aliambia Taifa Leo hapo Aprili 19.
Mabingwa hao wa Raga ya Dunia duru ya Singapore mwaka 2016 wameshiriki mashindano manne tangu Februari. Walimaliza katika nafasi ya pili nyuma ya Argentina mjini Madrid nchini Uhispania mnamo Februari 20-21 na Februari 27-28. Walitupwa hadi nambari ya tatu mjini Dubai mnamo Aprili 2-3 na katika nafasi ya tano mnamo Aprili 8-9.
Katika ziara za Uhispania na Dubai, Shujaa waliandamana na timu ya taifa ya kinadada ya Kenya maarufu kama Lionesses. Vipusa wa kocha Felix Oloo walivuta mkia Februari 20-21, Aprili 2-3 na Aprili 8-9 na nambari mbili mnamo Februari 27-28.
Shujaa na Lionesses wameratibiwa kuelekea mjini Los Angeles, Amerika kwa shindano la mwisho la kujipima nguvu baada ya ziara ya Afrika Kusini. Timu hizi zinajiandaa kwa Michezo ya Olimpiki itakayofanyika mjini Tokyo, Japan kutoka Julai 23 hadi Agosti 8.