Na GEOFFREY ANENE
TIMU ya taifa ya raga ya wachezaji saba kila upande ya wanaume maarufu kama Shujaa, mnamo Alhamisi ilichukua mapumziko ya siku moja kupata mafunzo ya uhodari wa kiakili katika uchezaji mzuri.
Shujaa ya kocha Innocent “Namcos” Simiyu itakabana koo na Amerika, Afrika Kusini na Ireland katika mechi za Kundi C za Olimpiki 2020 zitakazofanyika jijini Tokyo, Japan mnamo Julai 23 hadi Agosti 8.
“Vipindi vilivyoendeshwa na daktari Kanyali Ilako, vilikuwa muhimu katika kuhakikisha wachezaji wanapata kuwa na mtazamo mzuri uwanjani, hata wakati kuna presha,” Simiyu alieleza Taifa Leo kutoka mjini Kurume ambako timu hiyo imepiga kambi kwa matayarisho ya mwisho.
Nahodha huyo wa zamani wa Shujaa aliongeza kuwa timu hiyo imejaa motisha.
“Tumefaulu katika kupata nafuu tena baada ya kusumbuliwa na usingizi kutokana na tofauti ya kimaeneo katika saa,” alisema.
Japan iko saa sita mbele ya Kenya. Mnamo Jumanne, Shujaa ilipigwa jeki baada ya nyota William Ambaka kufika kambini akitokea klabu yake mpya ya Narvskaya Zastava nchini Urusi. Hapo Jumatano, Shujaa pia ilikuwa na kipindi cha kukandwa.
Nayo, timu ya kina dada maarufu Lionesses ilikuwa na kipindi chake cha kwanza cha mazoezi ya uwanjani.
Lionesses itamenyana na New Zealand, Urusi na Uingereza katika mechi za Olimpiki za Kundi A.