• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Shujaa yafunzwa umuhimu wa utimamu wa kiakili nao Lionesses wakianza mazoezi ya Olimpiki

Shujaa yafunzwa umuhimu wa utimamu wa kiakili nao Lionesses wakianza mazoezi ya Olimpiki

Na GEOFFREY ANENE

TIMU ya taifa ya raga ya wachezaji saba kila upande ya wanaume maarufu kama Shujaa, mnamo Alhamisi ilichukua mapumziko ya siku moja kupata mafunzo ya uhodari wa kiakili katika uchezaji mzuri.

Shujaa ya kocha Innocent “Namcos” Simiyu itakabana koo na Amerika, Afrika Kusini na Ireland katika mechi za Kundi C za Olimpiki 2020 zitakazofanyika jijini Tokyo, Japan mnamo Julai 23 hadi Agosti 8.

“Vipindi vilivyoendeshwa na daktari Kanyali Ilako, vilikuwa muhimu katika kuhakikisha wachezaji wanapata kuwa na mtazamo mzuri uwanjani, hata wakati kuna presha,” Simiyu alieleza Taifa Leo kutoka mjini Kurume ambako timu hiyo imepiga kambi kwa matayarisho ya mwisho.

Nahodha huyo wa zamani wa Shujaa aliongeza kuwa timu hiyo imejaa motisha.

“Tumefaulu katika kupata nafuu tena baada ya kusumbuliwa na usingizi kutokana na tofauti ya kimaeneo katika saa,” alisema.

Japan iko saa sita mbele ya Kenya. Mnamo Jumanne, Shujaa ilipigwa jeki baada ya nyota William Ambaka kufika kambini akitokea klabu yake mpya ya Narvskaya Zastava nchini Urusi. Hapo Jumatano, Shujaa pia ilikuwa na kipindi cha kukandwa.

Nayo, timu ya kina dada maarufu Lionesses ilikuwa na kipindi chake cha kwanza cha mazoezi ya uwanjani.

Wanaraga wa Kenya Lionesses wakifurahia kipindi chao cha kwanza cha mazoezi ya Olimpiki mjini Kurume, Japan mnamo Julai 15, 2021. Picha/ Hisani

Lionesses itamenyana na New Zealand, Urusi na Uingereza katika mechi za Olimpiki za Kundi A.

You can share this post!

Hofu ya Eunice Sum kuhusu kufifia kwa kina dada Wakenya...

Omar Lali mpenziwe marehemu Tecra Muigai aagizwa ahudhurie...