• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 6:40 PM
STAA WA SPOTI: Nguli wa fani ya soka nchini Kenya

STAA WA SPOTI: Nguli wa fani ya soka nchini Kenya

NA GEOFFREY ANENE

MICHAEL Olunga ni mshambulizi matata wa Kenya na klabu ya Al Duhail nchini Qatar.

Nyota huyo maarufu kama Engineer, aliibuka mfungaji bora kwenye Ligi Kuu ya Qatar (QSL) kwa mabao 24 katika msimu.

Alitajwa Jumanne katika kikosi cha wachezaji 11-bora wa raundi ya sita ya Klabu Bingwa Asia ukanda wa Magharibi alipochangia mabao mawili na kusuka pasi iliyojazwa kimiani wakati Al Duhail ilizima Sepahan kutoka Iran 5-2 katika Kundi D.

Nahodha huyo wa Harambee Stars alilelewa mtaani Lucky Summer jijini Nairobi. Alianzia uanasoka katika akademia ya Liberty jijini Nairobi.

Mwanafunzi huyo wa zamani wa Shule ya Upili ya Upper Hill alichezea Tusker FC 2012-2013 na kisha Thika United kwa mkopo kutoka Liberty.

Aliyoyomea Gor Mahia 2014-2015.

Alipata umaarufu kwa kasi yake na ustadi wa kukamilisha mashambulizi.

Olunga alifungia Gor magoli 19 msimu huo. Alizoa mataji ya Top 8 akiwa Tusker na Gor.

Pia, alishinda Ligi Kuu mara mbili akiwa Gor.

Tangu aanze kusakata soka ya malipo 2012, Olunga amejaza kimiani jumla ya mabao 127 katika michuano 190. Manne yamepatikana kwenye Klabu Bingwa msimu huu.

Mwanasoka huyo bora Kenya mwaka 2015 alianza kutandaza kabumbu katika mataifa ya kigeni 2016 alipojiunga Djurgarden (Uswidi) baada ya ombi lake kwa kocha Mfaransa Arsene Wenger amsaini kufeli.

Alichezea Zhicheng, Uchina iliyompeleka Hengfeng (Uchina) na Girona (Uhispania) kwa mkopo kabla ya kuingia Kashiwa Reysol, Japan kwa Sh346.7 milioni.

Alivuma sana akiwa kambini Kashiwa kwa miaka miwili na nusu. Alitwaa taji la Mfungaji Bora na Mchezaji Bora wa mwaka 2020.

Hakuna Mwafrika mwingine ameibuka Mchezaji Bora Japan tangu ligi hiyo ianzishwe 1993.Al Duhail ilimnyakua Januari 2021 kwa zaidi ya Sh700 milioni.

Aliibuka mfungaji bora Klabu Bingwa Asia 2021 alipochana nyavu mara tisa. Alishinda Kombe la Amir mnamo Machi 18. Olunga anaaminika kupokea mshahara wa Sh17 milioni kila mwezi kambini mwa Al Duhail.

You can share this post!

KCB yamwaga Sh70m kudhamini mbio za magari Uganda

Presha City ikizuru Leeds, Liverpool ikivizia Newcastle

T L