NA GEOFFREY ANENE
KENYA Commercial Bank (KCB) Uganda imemwaga Sh70 milioni kudhamini mbio za magari nchini Uganda ikiwemo duru ya Afrika ya Pearl Rally mnamo Mei 6-8.
Benki ya KCB, ambayo makao yake makuu ni jijini Nairobi, haijakuwa makini kudhamini mbio za magari za Kenya mwaka huu. Ilikuwa imefadhili mbio za magari Kenya kwa karibu Sh1.2 bilioni kati ya 2003 na 2021 kabla ya kuenda kimya msimu huu.
Imetangaza kupiga jeki fani hiyo nchini Uganda ambapo inarejea baada ya miaka 11.
Vyombo vya habari vya Uganda vimenukuu Afisa Mkuu wa Mauzo wa KCB Bank Uganda Diana Komukama Ssempembwa akisema anaamini kujitosa kwa benki hiyo katika fani hiyo ni mwanzo wa uhusiano mwingine na Shirikisho la Klabu la Mbio za Magari Uganda (FMU).
Madereva Karan Patel na Nikhil Sachania pamoja na chipukizi McRae Kimathi, Jeremy Wahome, Maxine Wahome na Hamza Anwar kutoka Kenya watawania taji la Pearl Rally ambayo ni duru ya tatu msimu huu baada ya Bandana nchini Ivory Coast na Equator Rally nchini Kenya.
Pearl Rally, ambayo imevutia jumla ya madereva 49, itajumuisha kilomita 513. Kilomita 212 zitakuwa za kuwania pointi na kilomita 197 zinazounganisha barabara za mashindano.