NA PATRICK KILAVUKA
ANASEMA anadhamini soka kwa sababu inaweza kumtoa mchezaji mavumbini mpaka awe mchezaji wa hadhi ya kutajika.
Anatoa mfano wa Lionel Messi ambaye alitia bidii kuhakikisha anaweka jina la taifa lake la Argentina kwenye ramani ya kimataifa baada ya kuwa nahodha wa timu ya taifa na kuhakikisha imepambana ukucha na jino kutwaa taji la Kombe la Dunia nchi Qatar mwaka 2022.
Hii ni baada ya kulelewa na akademia ya klabu ya Barcelona katika miaka ya awali kabla ya kuyoyomea kupunga unyunyu katika timu ya PSG na kusalia kifaa wembe.
Aidha, Messi ametia kapuni mataji kadha wa kadha likwemo la juzi la mchezaji bora wa dimba la Dunia.
Keycee Len,13, ni mwanafunzi wa shule ya Jabali Elementary iliyoko mkabala wa barabara ya Arboretum, jijini Nairobi.
Alianza soka akiwa na umri wa miaka mitatu katika chekechea. Alipotimu miaka saba, alijiunga na timu ya Soccer Talent Academy.
Kwa sababu alinuia kujiimarisha zaidi katika kabumbu, alisajiliwa na akademia ya Kibera Soccer Academy (KESA) miaka miwili iliyopita. Anakariri kwamba, ni baada ya kujiunga na akademia hii, ndipo nyota yake ya jaha katika mchezo ilianza kungaa pamoja na kujipanulia mbawa katika soka.
“Sababu ambazo zilimshawishi kujiunga na KESA ni kwamba, ina vifaa vya kandanda na makocha ambao wanafaa wanasoka kwa hali zote. Wao huwalea mithili ya mzazi aliye na mori na kiu ya kuona mwanawe anapata ufanisi katika maisha,” anasema mwanadimba huyo chipukizi ambaye aliyetawazwa mfungaji bora katika kipute cha UFA Cup.
Kipute hicho kinajumuisha akademia za soka ambazo jijini na nje ya nchi ikwemo Uganda.
Alitikisa nyavu mara nane na kupokea tuzo hiyo. Patashika hiyo iliandaliwa katika uga wa Chuo Kikuu cha Nairobi cha Lower Kabete, mnamo Desemba, 2022.
Chini ya kocha Aswani Clyde, anaungama kwamba amefinyangwa kuwa winga wa kushoto na kulia.
Anadokeza kwamba, kocha amemwelekeza katika kujifunza kupiga pasi za uhakika,miguso ya boli kwa weledi, kupiga frikiki na kufuma magoli.
Mchezaji huyu wa pembeni anakariri kwamba amejiongezea ujuzi kutokana na mchezaji Messi kwani, anapomtazama runingani akifanya vimbwanga vyake vya kusakata boli kwa weledi, nidhamu na umakinifu, humfungua zaidi katika kusakata boli.
“Messi hunifurahisha na chenga za maudhi, pasi nyerezi na za uhakika ambazo huzua rabsha malangoni na hata kusababisha mabao. Isitoshe, yeye huvutiwa sana na ulimaji wake wa penalti au frikiki ambao huwaacha makipa vinywa wazi nyavu zikitikiswa,” aongeza Len.
Anawapongeza wadau wa timu ya KESA na wazazi wake ambao wamemwezesha kupata fursa ya kuhudhuria mazoezi na kusimama naye katika ari ya kusuka talanta yake ambayo anakariri kwamba, itamfaa kwa sasa na siku za majaliwa.
Anashauri wenye ndoto kama yake kwamba, njia pekee ya kujikuza katika kipaji hiki ni kwa kutia bidii, kujifunga kibwebwe na kujitolea mhanga kutimiza ndoto uliyo nayo. Hivyo basi, ni vyema kuwa mwenye nidhamu na bidii.
Subscribe our newsletter to stay updated