NA GEOFFREY ANENE
WACHEZAJI 120 wamethibitisha kushiriki mashindano ya tenisi ya Ferdinand Omanyala 10s yatakayoleta pamoja watoto kutoka umri wa miaka minne hadi 12 mnamo Jumamosi.
Shirikisho la Tenisi Kenya limesema mashindano hayo yataandaliwa uwanjani Nairobi Club. Yataanza saa tatu asubuhi na kukamilika saa tisa alasiri siku hiyo.
Mshikilizi wa rekodi ya Afrika mbio za mita 100 Omanyala, ambaye mwaka huu 2022 pia ameshinda mataji ya Kip Keino Classic, Riadha za Afrika na michezo ya Jumuiya ya Madola, ni balozi wa mradi wa tenisi ya chipukizi nchini Kenya (JTI). Analenga kupatia motisha kizazi cha wachezaji walio na umri mdogo.
Bingwa wa Kenya Open 2018 na Afrika U18 2021 Angella Okutoyi,18, aliyeshinda mataji ya wachezaji wawili kila upande ya chipukizi ya Wimbledon na J1 Repentigny, pia atahudhuria.