• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 4:23 PM
UDAKU: Kipendacho roho ya Rashford ni Lucia tu!

UDAKU: Kipendacho roho ya Rashford ni Lucia tu!

IMEKUSANYWA NA CHRIS ADUNGO

HATIMAYE fowadi wa Manchester United, Marcus Rashford, amerudiana na mchumba wake wa tangu utotoni, Lucia Loi.

Wawili hao wanaanza tena kutoka kimapenzi baada ya miezi minane ya kutengana.

Lucia alionekana pamoja na Rashford wiki hii katika mkahawa mmoja wa kifahari jijini Manchester, Uingereza, wakiponda raha ya ujana. Gazeti la The Sun limebaini kwamba videge hao walipatanishwa na familia zao mnamo Disemba 24, 2021.

Baadhi ya picha walizopigwa katika kikao hicho cha faragha zilisambazwa mitandaoni mnamo Januari 3, 2022 baada ya kukamilika kwa mechi ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) iliyoshuhudia Wolves iking’ata Man-United 1-0 ugani Old Trafford.

Kwenye picha moja, Lucia alionekana akipanda gari jeusi linaloaminika kuwa la Rashford.

Alikuwa ameshikwa kiunoni na mkono uliokuwa umechanjwa chale ambazo zinaaminika kuwa za fowadi huyo wa timu ya taifa ya Uingereza.

“Hawa ni watu wawili wenye historia ndefu pamoja. Penzi limewaunganisha tena. Lucia ni miongoni mwa watu wanaoelewa Rashford kwa undani. Walipatana kabla ya Krismasi na watafunga ndoa hivi karibuni,” akasema Melanie Maynard ambaye ni mamake Rashford.

Lucia ambaye ni afisa wa uhusiano mwema katika kampuni moja ya sukari nchini Uingereza, amekuwa nguzo muhimu katika safari ya kuimarika kwa Rashford kitaaluma.

“Nia yao ya kurudiana imekuwapo tangu awali. Kutengana kuliwapa fursa ya kufahamu nguvu za penzi lao. Kila mmoja anajua thamani ya mwenzake. Wanastahiana kwa penzi la dhati na wanaaminiana sana,” akaongeza Melanie ambaye amekuwa mstari wa mbele kupatanisha Rashford na Lucia.

Sawa na Lucia, Rashford pia ana umri wa miaka 24.

Walianza kutambaliana kimapenzi mnamo 2013 wakiwa wanafunzi katika Shule ya Mersey, eneo la Ashton, jijini Manchester.

Alianza kuvalia jezi za kikosi cha kwanza cha Man-United mnamo 2016 akiwa na umri wa miaka 18 pekee na akafunga mabao mawili dhidi ya Arsenal katika mchuano wake wa kwanza.

Baada ya kutengana mnamo Mei 2021, Lucia alifuta mitandaoni picha zote alizopigwa na Rashford, jambo ambalo Melanie anakiri liliathiri mwanawe kisaikolojia na kuchangia kushuka kwa makali yake kambini mwa Man-United.

Kwa mujibu wa msemaji wa familia ya Rashford, kiini cha kusambaratika kwa uhusiano wake na Lucia ni presha iliyochangiwa na kanuni kali za ‘lockdown’ katika juhudi za Uingereza kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona.

“Rashford alikosa utulivu. Aliumia sana kimawazo tangu Lucia afunganye virago na kujiendea zake. Uhusiano wao ulivurugwa na ‘lockdown’ ambayo iliwaweka katika ulazima wa kuishi pamoja kwa mara ya kwanza kwa zaidi ya miezi 12. Bila shaka walitofautiana kifikra kuhusu mambo fulani,” akaeleza.

“Kutengana kwao hakukuhusisha mtu yeyote. Waliachana kwa uzuri na wakaendelea kuwasiliana. Wangali wachanga na wako katika mwanzo wa safari ambayo sasa itaishia kwa ndoa,” akaongeza.

Lucia ambaye amefanya kazi nyingi za hisani nchini Zambia na Sri Lanka, amekuwa akiunga mkono miradi mingi ya Rashford ambaye amekuwa akipigana dhidi ya umaskini na kutetea haki za watoto kupata chakula na elimu.

You can share this post!

Raia wa Congo anayeshtakiwa kwa ulaghai wa Sh105Milioni...

WANDERI KAMAU: Uhuru amwige Suluhu ili kulainisha serikali...

T L