• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:10 PM
Ujerumani yakomoa Iceland 3-0

Ujerumani yakomoa Iceland 3-0

Na MASHIRIKA

KAI Havertz na Ilkay Gundogan walifunga bao kila mmoja na kusaidia Ujerumani kuanza vyema kampeni zao za kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2022 kwa kuwapepeta Iceland 3-0 mnamo Alhamisi usiku.

Ujerumani waliokuwa wenyeji wa mechi hiyo, walipachika wavuni mabao mawili ya haraka chini ya dakika saba za ufunguzi wa kipindi cha kwanza.

Havertz ambaye ni fowadi wa Chelsea, alifungia Ujerumani goli la pili baada ya ukurasa wa magoli kufunguliwa na kiungo matata wa Bayern Munich, Leon Goretzka katika dakika ya tatu.

Gundogan ambaye ni kiungo wa Manchester City, alizamisha kabisa chombo cha Iceland kwa kufungia Ujerumani goli la tatu katika dakika ya 56.

Gundogan kwa sasa amepachika wavuni jumla ya mabao 15 kutokana na mechi 24 zilizopita katika ngazi ya klabu na timu ya taifa.

Iceland walionekana kuzidiwa maarifa na Ujerumani katika takriban kila idara na jaribio la pekee walilolipata langoni mwa wenyeji wao ni kombora kutoka kwa Runar Sigurjonsson.

Ujerumani wangalifunga idadi kubwa zaidi ya magoli katika mechi hiyo ila wakapoteza nafasi nyingi za wazi walizozipata kupitia kwa Timo Werner, Jamal Musiala na Antonio Rudiger.

Kocha Joachim Loew ambaye ataagana rasmi na kikosi cha Ujerumani mwishoni mwa kampeni za Euro 2021, aliridhishwa na matokeo ya masogora wake.

Ujerumani kwa sasa watakuwa wageni wa Romania katika mchuano wa pili wa Kundi J huku Iceland wakiwaendea Armenia mnamo Jumapili ya Machi 28, 2021.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

AKILIMALI: Jinsi unavyoweza kuzalisha mparachichi kutoka...

Uhispania wakabwa koo na Ugiriki