• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Ulinzi Starlets walenga kutwaa taji la KWPL msimu ujao

Ulinzi Starlets walenga kutwaa taji la KWPL msimu ujao

NA TOTO AREGE

KOCHA wa wanajeshi wa Ulinzi Starlets Joseph Mwanzia amepongeza warembo hao kwa kupiga Nakuru City Queens 3-1 katika fainali ya Kombe la Wanawake la Shirikisho la Soka nchini (FKF) ugani Nyayo jijini Nairobi mnamo Jumapili.

Katika mechi hiyo, washambulizi Mercy Airo na Neddy Atieno walifunga mabao mawili na moja mtawalia katika mechi hiyo.

Mshambulizi Fasila Adhiambo alikuwa mfungaji bora wa Ulinzi kwenye mashindano ya kombe hilo akiwa na mabao manane.

Ulinzi walishinda makala ya kwanza ya shindano hilo mwaka wa 2021 baada ya kuwalaza Vihiga Queens 2-0 kwenye fainali iliyosakatwa katika Uwanja wa Maonyesho ya Kilimo, Kaunti ya Nakuru.

Pia, Ulinzi ndio mabingwa wa kombe la FKF la Super ambalo walishinda mwaka uo huo.

Kocha Mwanzia anasema Ulinzi sasa wanalenga kupigania ubingwa wa Ligi Kuu ya Wanawake Nchini (KWPL) msimu ujao.

“Tumeshinda makombe yote katika soka ya wanawake na sasa limesalia kombe moja tu ambalo ni la ligi. Msimu huu kidogo tu tulipate lakini likatutoka mwishoni mwa msimu,” alisema Mwanzia.

Wanajeshi hao walimaliza nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Wanawake (KWPL) na alama 45. Alama 10 nyuma ya mabingwa ligi Vihiga Queens.

“Tunaheshimu wapinzani wetu lakini msimu ujao watusamehe. Ninajua watakuwa wamejipanga lakini pia sisi tutakuwa tumejipanga zaidi. Lengo letu msimu ujao ni kuchukua ubingwa wa ligi,” aliongezea Mwanzia.

  • Tags

You can share this post!

Kaunti ya Nyamira yamulikwa kwa kuajiri wafanyakazi wote...

Kindiki atarajiwa kufungua rasmi awamu ya tatu ya ufukuaji...

T L