Na GEOFFREY ANENE
MKENYA Vicoty Chepng’eno ameibuka malkia mpya wa mbio za Houston Half Marathon nchini Amerika, Jumapili.
Chepng’eno amekamilisha mbio hizo za kilomita 21 kwa saa 1:05:03 akivunja rekodi ya Houston Half Marathon ya saa 1:05:50 ambayo Mkenya mwenzake Brigid Kosgei aliweka akitwaa taji la mwaka 2019.
Pia, Chepng’eno pia ameimarisha muda wake bora kutoka 1:07:22 ambao aliweka akinyakua taji la Philadelphia Half Marathon mwezi Novemba 2021.
Chepng’eno, 28, amefuatiwa kwa karibu na Mwamerika Sarah Hall (1:07:15).
Taji la wanaume limenyakuliwa na Muethiopia Milkesa Tolosa kwa saa 1:00:24, huku Wakenya John Korir na Wilfred Kimitei wakiridhika na nafasi mbili zilizofuata kwa saa 1:00:26 na 1:00:43 mtawalia.
Mwamerika Kirubel Erassa alikamata nafasi ya nne kwa 1:00:44 naye Mkenya Shadrack Kimining akafunga mduara wa tano-bora kwa 1:00:53. Mwanamume wa mwisho kutoka Kenya kushinda Houston Half Marathon ni Nicodemus Malakwen mwaka 2006.