• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 11:39 AM
Vihiga Queens wajikatia tiketi ya kulimana na Simba Queens

Vihiga Queens wajikatia tiketi ya kulimana na Simba Queens

Na GEOFFREY ANENE

WENYEJI Vihiga Queens wametinga nusu-fainali ya mashindano ya Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) ya kufuzu kushiriki Klabu Bingwa Afrika ya kinadada baada ya kulima New Generation kutoka Zanzibar 8-0 ugani Nyayo, Ijumaa.

Jentrix Shikangwa alitetemesha nyavu za Generation mara tatu, Tereza Engesha mara mbili nao Mercy Anyango, Robai Kebedi na Maureen Achieng’ wakachangia bao moja kila mmoja katika mechi hiyo ya mwisho ya Kundi B.

Vipusa wa kocha Charles Okere na Boniface Nyamunyamu walijikatia tiketi kwa kumaliza Kundi B katika nafasi ya pili kwa alama sita, tatu nyuma ya wanabenki wa CBE kutoka Ethiopia waliolipua Yei Joint Stars kutoka Sudan Kusini 10-0.

Vihiga watamenyana na washindi wa Kundi A Simba Queens katika nusu-fainali mnamo Septemba 6 nao CBE watalimana na Lady Doves kutoka Uganda waliokamilisha Kundi A katika nafasi ya pili kwa tofauti ya ubora wa magoli baada ya wote kutoshana kwa pointi saba kila mmoja. Lady Doves walilima PVP kutoka Burundi 3-0 Septemba 3.

Yei na Generation wamebanduliwa kutoka Kundi B nao PVP na FAD kutoka Djibouti wameaga mashindano kutoka Kundi A. Washindi wa Cecafa pekee watafuzu kushiriki Klabu Bingwa Afrika baadaye mwaka huu wa 2021 nchini Misri.

  • Tags

You can share this post!

Polisi 6 wakanusha mauaji ya ndugu wawili wa Kianjokoma

Mjukuu wa Moi akubali watoto aliokana awali