Na JOHN KIMWERE
TIMU za wanawake za Kenya Prisons, Kenya Pipeline na KCB Bank ziliwasili vyema nchini Tunisia tayari kushiriki kampeni za voliboli ya Klabu Bingwa Afrika (CAVB) muhula huu.
Kocha wa Kenya Pipeline, Paul Gitau na mwenzake wa Kenya Prisons, Josp Barasa walisema kuwa wamepania kumaliza kati ya nafasi tatu bora mwaka huu.
Kwenye kipute cha mwaka 2021, Kenya Prisons ilimaliza katika nafasi ya tatu nayo Kenya Pipeline iliibuka ya tano.
‘Tumekuwa na maandalizi mema ambapo wasichana wangu wako tayari kupambana na wapinzani wao kwenye kinyang’anyiro cha mwaka huu,” kocha wa Kenya Prisons alisema na kushukuru kampuni ya Hass Petroleum ambayo imejivika jukumu la udhamini wa mavazi watakayovalia kwenye mechi za pambano hilo.
Kocha wa Kenya Pipeline, Paul Gitau alisema: ”Kusema ukweli tunashukuru uongozi wa Kenya Pipeline umetupatia nafasi kushiriki kipute hicho ili tuzidi kupaisha Kenya kimataifa katika mchezo wa voliboli.”
Kenya Prisons mabingwa wa Ligi Kuu nchini wanajivunia huduma za nahodha Blackcides Agala, Pamela Jepkirui, Yvonne Wavinya, Joan Chebet, Ann Lowem, Emmaculate Chemutai na Sheila Khasandi Jipukisi kati ya wengine.
Rose Magoi na Gladys Ekaru Emaniman ndio watakuwa nahodha na naibu wa nahodha wa Kenya Pipeline.