• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Wales wazamisha chombo cha Uturuki kwa ushindi wa 2-0 kwenye Euro

Wales wazamisha chombo cha Uturuki kwa ushindi wa 2-0 kwenye Euro

Na MASHIRIKA

WALES waliwapepeta Uturuki 2-0 katika mechi ya Kundi A kwenye Euro mnamo Jumatano usiku jijini Baku, Azerbaijan na kujiweka pazuri zaidi kuingia katika hatua ya 16-bora ya kipute hicho.

Wales walianza mchuano huo uliohudhuriwa na zaidi ya mashabiki 30,000 kwa matao ya juu huku wakilenga kuendea mabao ya mapema.

Hata hivyo, nahodha Gareth Bale alipoteza nafasi nyingi za wazi kabla ya kiungo Aaron Ramsey wa Juventus kuwaweka Wales kifua mbele katika dakika ya 42.

Japo Uturuki walianza vyema kampeni zao za kipindi cha pili kupitia mashambulizi ya Merih Demiral aliyemtatiza kipa Danny Ward, walishindwa kuvuruga mpango wa Wales waliosalia thabiti katika safu ya kati.

Bale aliyechangia mabao yote mawili ya Wales alipoteza penalti aliyopata katika dakika ya 61 kwa kupaisha mpira juu ya mwamba wa goli la Uturuki.

Hata hivyo, alishirikiana vilivyo na Connor Roberts aliyepachika wavuni goli la pili la Wales mwishoni mwa kipindi cha pili.

Wales walioambulia sare ya 1-1 dhidi ya Uswisi katika mchuano wa ufunguzi mnamo Juni 12, sasa wanadhibiti kilele cha Kundi A kwa alama nne. Kikosi hicho kitavaana na Italia katika mechi ya mwisho ya makundi mnamo Juni 20 jijini Roma huku Uturuki wakikamaliza udhia dhidi ya Uswisi jijini Baku.

Uturuki kwa sasa wanavuta mkia wa Kundi A bila alama yoyote baada ya Italia kuwapokeza kichapo cha 3-0 katika mchuano wa ufunguzi wa Kundi A mnamo Juni 11, 2021 uwanjani Olimpico, Italia.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Vita vya Obado dhidi ya Raila, ODM vingalipo

Masika na Vissel Kobe wanyeshea Suzuka Point Getters kipute...