• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 11:53 AM
Wanavoliboli wa KU wajiandaa kushiriki voliboli ya Kombe la Dunia FISU

Wanavoliboli wa KU wajiandaa kushiriki voliboli ya Kombe la Dunia FISU

NA JOHN KIMWERE

TIMU ya wanaume ya voliboli ya Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU) maarufu Assassins inajiandaa kukabili wapinzani wengine kwenye fainali za Kombe la Dunia (FISU) mwaka 2023.

Wanazuo hao walifuzu kushiriki ngarambe hiyo itakayoandaliwa nchini China, baada ya kumaliza nafasi ya pili kwenye shindano la Vyuo Vikuu vya Afrika (FASU) lililofanyika kwenye chuo hicho mwezi Juni 2022.

Wanaume hao chini ya nahodha, James Mwaruwa walimaliza nafasi ya pili baada ya kushindwa kwa seti 3-0(25-20, 25-23, 25-23) na America International University of Cairo (AIU) ya Misri kwenye mechi ya kwanza.

Kwenye mechi ya pili KU ilishinda kwa seti 3-1 (22-25, 25-22, 25-20, 35-33).

Kwa ujumla AIU iliibuka mabingwa kwa idadi ya seti.

“Itakuwa mara ya kwanza KU kushiriki kipute hicho ambapo tunafahamu bayana kuwa tunatarajia ushindano mkali dhidi ya wapinzani wengine hasa timu kutoka mataifa ya Bara Ulaya ikiwamo wenyeji Uchina kati ya nyingine,” amesema kocha wa KU, Vitalis Ojukwu na kuongeza kuwa watajitahidi kiume kuonyesha uwezo wao kwenye fani hiyo.

Kocha wa Assassins akiwa na wachezaji wake. PICHA | JOHN KIMWERE

Anakariri kuwa kando na kushiriki kipute hicho wanajiandaa kutetea ubingwa wa Afrika Mashariki na Kati (EAUG) walioshinda mwaka 2016. Ngarambe hiyo itafanyika nchini Uganda mwishoni mwa mwaka huu.

KU inajivunia kushinda mataji kadhaa kwenye michezo ya Vyuo Vikuu vya Kenya (KUSF) Kanda ya Nairobi na kubanduliwa mara kadhaa kwenye fainali za kitaifa.

Kocha huyu anajivunia kunoa timu tofauti za vyuo vikuu, klabu za mitaani vya mchezo huo, Shule za Msingi na Shule za sekondari kwa kipindi cha miaka 15 huku ikiwa ni mwaka wa saba akinoa kikosi hicho.

Amehitimu kama kocha na mwamuzi wa voliboli kiwango cha kitaifa (KVF) daraja la kwanza na pili pia kimataifa (FIVB) daraja la kwanza.

Pia katika voliboli ya walemavu amehitimu kama kocha na mwamuzi pia amehitimu kwa diploma kwenye mchezo huo kiwango cha kimataifa.

Kwenye mchezo wa floorball amehitimu kama kocha na refarii pia amehitimu kwa viwango hivyo kwenye fani ya Rollball.

“Bila shaka kwa jumla ninashukuru menejimenti ya KU kwa kufadhili vikosi vya michezo tofauti ambapo wachezaji hutumia wakati huo kukuza talanta zao,” akasema na kutoa wito kwa vyuo vingine kuiga mtindo bila kulegeza kamba.

Kocha wa Assassins akiongea na wachezaji wake. PICHA | JOHN KIMWERE

Anataka serikali ishirikiane na Shirikisho la Voliboli ya Kenya (KVF) kujenga kumbi za mchezo huo katika Kaunti zote ili kutia wachezaji chipukizi motisha kunoa talanta zao.

Anatoa wito kwa KVF iwazie kuanzisha ligi za viwango vya chini: Ligi ya Taifa Daraja la Kwanza na Pili ili kutoa mwanya kwa timu za shule na vyuo vikuu kushiriki ambapo wachezaji wengi watapata nafasi kupalilia talanta zao.

Kwa hicho kinajumuisha wachezaji kama: James Mwaruwa na Stephen Ogello (nahodha na naibu wake, Ian Omondi, Kevin Kiptanui, Steven Otieno, Edwin Obuya, Boaz Oduor, Joshua Boso, Davies Mutie, Alfred Neko, Brian Mwangi, Oscar Juma, Davies Kimaru na Erick Otieno.
  • Tags

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Teknolojia ya uchaguzi IEBC ingefanywa na...

Hoki: Titans yajipatia miaka 5 ili kushiriki kipute cha...

T L