Na MASHIRIKA
KOCHA Ralph Hasenhuttl amesema wanasoka wake wa Southampton walizawidiwa kutokana na “ujasiri” waliodhihirisha katika ushindi wa 3-2 dhidi ya West Ham United kwenye mchuano wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mnamo Jumapili uwanjani London Stadium.
Jan Bednarek aliyefunga bao la pili kutokana na mechi tatu aliongoza Southampton kusajili ushindi wao wa kwanza baada ya kutandaza mechi saba za EPL.
Kwa upande wao, West Ham wanaotiwa makali na kocha David Moyes sasa wamesakata mechi tano za EPL bila kuvuna ushindi. Ingawa walitoka nyuma mara mbili na kusawazisha dhidi ya Southampton, juhudi zao ziliambulia pakavu.
“Huu ni ushindi mkubwa kwa Southampton ambao hawakuwa wamewahi kuondoka uwanjani London Stadium na alama yoyote chini ya kipindi cha miaka mitano iliyopita,” akasema Hasenhuttl.
“Tulicheza vyema leo na tukajiamini zaidi baada ya kufunga bao la kwanza na kikosi kizima kikajituma marudufu bila uoga hata baada ya wenyeji wetu kusawazisha,” akaongeza kocha huyo.
Mohamed Elyounoussi aliwaweka Southampton kifua mbele katika dakika ya nane baada ya kumwacha hoi kipa Lukasz Fabianski aliyetatizwa pia na kiungo Kyle Walker-Peters.
Ingawa Michail Antonio alisawazishia West Ham mwanzoni mwa kipindi cha pili, James Ward-Prowse aliwarejesha Southampton uongozini katika dakika ya 61 kabla ya Said Benrahma kusawazishia West Ham dakika tatu baadaye. Beki Bednarek alifungia Southampton bao la ushindi katika dakika ya 70.
Bao la Antonio lilikuwa lake la kwanza baada ya mechi 10. Kichapo kutoka kwa Southampton kiliwateremsha West Ham hadi nafasi ya sita jedwalini kwa alama 28, nane zaidi kuliko Southampton ambao wanajivunia idadi sawa ya pointi na Crystal Palace na limbukeni Brentford.
MATOKEO YA EPL (Jumapili):
Man-City 6-3 Leicester
Norwich 0-5 Arsenal
Tottenham 3-0 Palace
West Ham 2-3 Southampton
Aston Villa 1-3 Chelsea
Brighton 2-0 Brentford
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO