• Nairobi
  • Last Updated May 10th, 2024 1:50 PM
West Ham yacharaza Lyon na kutinga nusu-fainali za soka ya bara Ulaya

West Ham yacharaza Lyon na kutinga nusu-fainali za soka ya bara Ulaya

Na MASHIRIKA

WEST Ham United watamenyana na Eintracht Frankfurt ya Ujerumani katika nusu-fainali ya Europa League msimu huu baada ya kung’oa Olympique Lyon ya Ufaransa kwa jumla ya mabao 4-1 katika hatua ya nane-bora mnamo Aprili 14, 2022 nchini Ufaransa.

Baada ya kulazimishiwa sare ya 1-1 katika mkondo wa kwanza wa robo-fainali jijini London, Uingereza, West Ham ya kocha David Moyes ilikuwa na mlima mrefu wa kukwea ili kuingia nne-bora.

Craig Dawson alijaza kimiani krosi ya Pablo Fornals katika dakika ya 38 na kuweka West Ham uongozini. Declan Rice alifunga bao la pili la kikosi hicho mwishoni mwa kipindi cha kwanza kabla ya Jarrod Bowen kufanya mambo kuwa 3-0 katika dakika ya 48.

Mara ya mwisho kwa West Ham kunogesha nusu-fainali ya soka ya bara Ulaya ilikuwa miaka 46 iliyopita. Sasa wanakabiliwa na Frankfurt ya Ujerumani iliyobandua Barcelona ya Uhispania kwa jumla ya mabao 4-3 baada ya kuvuna ushindi wa 3-2 katika mchuano wa mkondo wa pili mnamo Alhamisi ugani Camp Nou.

West Ham waliwahi kukutana na Frankfurt kwenye nusu-fainali za European Cup Winners’ Cup mnamo 1976 na wakaibuka na ushindi wa 4-3.

Lyon ambao kwa sasa wanakamata nafasi ya 10 kwenye msimamo wa jedwali la Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1), hawakuwa wamepoteza mechi yoyote kati ya tisa za awali kwenye Europa League muhula huu wa 2021-22.

You can share this post!

Wawaniaji wa kujitegemea wataka muungano wao usajiliwe

Leicester yapepeta PSV na kuingia 4-bora Europa League

T L