• Nairobi
  • Last Updated May 10th, 2024 7:55 PM
Leicester yapepeta PSV na kuingia 4-bora Europa League

Leicester yapepeta PSV na kuingia 4-bora Europa League

Na MASHIRIKA

KIUNGO James Maddison amesema kikosi anachokichezea cha Leicester City kinalenga sasa kuweka historia kwa kunyanyua taji la Europa League baada ya kubandua PSV Einhoven ya Uholanzi kwa mabao 2-1 katika robo-fainali iliyochezewa uwanjani Philips.

Ni mara ya kwanza kwa Leicester kufuzu kwa nusu-fainali za soka ya bara Ulaya. Kikosi hicho kinachonolewa na kocha Brendan Rodgers kilishuka dimbani kikilenga ushindi wa angalau bao moja kwa nunge ili kusonga mbele baada ya kuambulia sare tasa katika mchuano wa mkondo wa kwanza mnamo Aprili 7, 2022 ugani King Power.

Leicester City sasa watakutana na AS Roma ya kocha Jose Mourinho iliyodengua Bodo/Glimt ya Norway kwa jumla ya mabao 5-2. Eran Zahavi alichuma nafuu kutokana na masihara ya Youri Tielemans na kufungia Leicester bao la kwanza kabla ya Maddison kusawazisha mambo kunako dakika ya 77.

Bao lililovunia Leicester ushindi lilifumwa kimiani na Ricardo Pereira dakika mbili kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mchezo kupulizwa. “Tuna kiu ya kuweka historia. Kikosi kinajituma vilivyo na jambo hilo linaridhisha. Tulicheza vizuri dhidi ya PSV na tuna kiu ya kushinda taji la Europa League ambalo litakuwa zawadi nzuri kwa mashabiki wetu,” akasema Maddison.

Chini ya kocha Rodgers, Leicester walijinyanyulia Kombe la FA mnamo 2020-21 baada ya kuzoa ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) chini ya mkufunzi Claudio Ranieri mnamo 2015-16.

Kwa kushinda taji la Europa League, Leicester watajikatia tiketi ya kushiriki soka ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) muhula ujao wa 2022-23. Kufikia sasa, kikosi hicho kinashikilia nafasi ya tisa kwenye msimamo wa jedwali la EPL kwa alama 40 huku pengo la pointi 17 likitamalaki kati yao na nambari nne Tottenham Hotspur.

PSV walijibwaga ugani wakipigiwa upatu wa kuzamisha chombo cha Leicester kwa urahisi baada ya kusakata jumla ya mechi 15 bila kupoteza. Aidha, hawakuwa wamefungwa bao katika mechi sita za awali chini ya mkufunzi Roger Schmidt.

You can share this post!

West Ham yacharaza Lyon na kutinga nusu-fainali za soka ya...

Raha muogeleaji Mkenya Kalombo akinyakua dhahabu Afrika...

T L