• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Ghasia katika kampeni za UDA

Ghasia katika kampeni za UDA

JOSEPH OPENDA na FRANCIS MUREITHI

KAMPENI za chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika uchaguzi mdogo wa udiwani katika wadi ya London, mjini Nakuru, jana ziligeuka uwanja wa fujo baada ya polisi kurusha vitoa machozi kwa msafara ulioongozwa na Seneta Susan Kihika.

Msafara huo ulikuwa ukimpigia debe Bw Anthony Nzuki, anayewania udiwani katika wadi hiyo kwa tiketi ya UDA.Kufuatia patashika hiyo, barabara ya Kenyatta Avenue iligeuzwa kuwa jukwaa la makabiliano, baada ya polisi waliojihami vikali kuzuia magari kwenye msafara huo kuingia katikati mwa mji huo.

Wenyeji walijipata pabaya baada ya magari ya polisi kufika kwa kasi kwenye barabara hiyo yakiwa tayari kukabili hali yoyote ambayo ingetokea. Hata hivyo, msafara haukusimama kwenye barabara hiyo, hasa baada ya kurushiwa gesi awali kwenye wadi hiyo.

Polisi walichukua udhibiti wa Barabara ya Gusii, huku wengine wakielekea katika Barabara ya Oginga Odinga kuwazuia wanasiasa waliokuwa msafarani dhidi ya kuingia eneo la kati mwa jiji.Masaibu ya wanasiasa na wafuasi wao yalianza wakati walikutana katika mtaa wa Milimani na kujaribu tena kuingia katikati mwa mji.

Majibizano yalizuka kati ya polisi na viongozi hao, ndipo wakalazimika kuwarushia vitoa machozi ili kuutawanya umati ulioandamana nao.Wengine waliokuwa kwenye msafara huo ni Mbunge wa Bahati, Kimani Ngunjiri.

Kamanda wa Polisi katika Kaunti Ndogo ya Nakuru Magharibi, Samson Gathuku, alisema polisi hawakuwa wamefahamishwa kuhusu mkutano huo.

“Hatukupata habari yoyote kuhusu mkutano uliopangwa. Bado tunatekeleza masharti ya serikali kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona,” akasema.Baada ya kutawanywa, wanasiasa hao walilazimika kuandaa mkutano wao kwenye makazi ya kibinafsi.Bi Kihika aliwalaumu polisi kwa kutumia nguvu kupita kiasi kuvuruga mkutano wao.

You can share this post!

JAMVI: Nyachae alivyomtayarisha Matiang’i kuwa...

Wajomvu sasa wataka warudishiwe ardhi yao