BENSON MATHEKA Na WINNIE ONYANDO
TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini (IEBC) imekataa orodha ya uteuzi ya vyama 79 vya kisiasa ikisema vyama hivyo havikuzingatia sheria.
Kulingana na tume hiyo, vyama hivyo vilikiuka sheria kwa kuwasilisha orodha zilizokuwa na dosari kwa kutozingatia ushirikishi.
Nafasi za wawakilishi wa kuteuliwa katika bunge la kitaifa, seneti na mabunge ya kaunti hutengewa makundi maalumu kama vile jamii ndogo, watu wanaoishi na ulemavu na vijana.
Hata hivyo, vyama viliorodhesha wanasiasa na maafisa wake, wakiwemo washirika wa viongozi wake.
Tume ilisema mbali na kukiuka sheria, vyama viliwasilisha orodha hizo kuchelewa.
Tume ilipatia vyama siku saba kurekebisha orodha hizo na kuziwasilisha upya kwa kuzingatia sheria.
Vyama hivyo sasa vina hadi Julai 22 kuwasilisha orodha zilizorekebishwa na kutimiza mahitaji ya sheria.
“Baada ya kupokea orodha iliyorekebishwa, tume itachapisha orodha hizo kwenye gazeti rasmi na kukaribisha malalamishi yoyote kutoka kwa vyama au wahusika,” ikasema IEBC.