• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 3:07 PM
JAMVI: Mirindimo mipya ya Tangatanga baada ya BBI kuzikwa

JAMVI: Mirindimo mipya ya Tangatanga baada ya BBI kuzikwa

Na WANDERI KAMAU

MRENGO wa ‘Tangatanga’ umepata msisimko mpya wa kisiasa katika ukanda wa Mlima Kenya na Bonde la Ufa, kufuatia uamuzi wa Mahakama Kuu kufutilia mbali mchakato wa Mpango wa Maridhiano (BBI).

Mara tu baada ya uamuzi huo, Naibu Rais William Ruto alitoa ujumbe “kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuipenda Kenya.”Dkt Ruto alisema huu ni wakati nchi iheshimu maamuzi yanayotolewa na taasisi huru.

Sherehe hizo zilitanda katika maeneo ya Kati, hasa Kaunti za Muranga, Nyeri na Nyandarua, viongozi wa mrengo huo wakiwaongoza wafuasi wao “kusherehekea” ushindi.Wabunge wanaoegemea mrengo huo walisema hatimaye mahakama imedhihirisha kuwa wao ndio “watetezi halisi” wa wananchi.

“Huu ni uamuzi unaooyesha wazi sisi ndio watetezi halisi wa wananchi. BBI ni njama na mpango wa watu wachache kujitengeneze nyadhifa za uongozi. Kama ambavyo tumekuwa tukishikilia, huu ni wakati kwa viongozi na serikali kuangazia masuala ya maendeleo na kufufua uchumi wa nchi. Mageuzi ya kikatiba ni jambo tunaloweza kushughulikia baadaye,” akasema mbunge Ndindi Nyoro (Kiharu) ambaye ni miongoni mwa washirika wakuu wa karibu wa Dkt Ruto.

Kauli kama hizo zilitolewa na wabunge Rigathi Gachagua (Mathira), Faith Gitau (Nyandarua), Milicent Omanga (Seneta Maalum) kati ya wengine ambao walikuwa miongonu mwa wale waliopiga kura ya ‘La.’

Katika kaunti za Baringo, Uasin Gishu na maeneo mengine ambayo ni ngome za kisiasa za Dkt Ruto, wananchi pia walijumuika pamoja kushabikia uamuzi huo.

Bunge la Kaunti ya Baringo lilikuwa miongoni mwa yale yalipiga kura kupinga mswada huo.Licha ya msisimko huo, wadadisi wa siasa wanasema kuwa ingawa huenda hilo likaonekana kama “ushindi” kwa wakati huu, bado ni mapema kwa mrengo huo kuanza kusherehekea.

Wanasema ingali mapema kudhani mchakato huo umevurugika kabisa, kwani bado kuna nafasi kwa wale wanaouendesha kuakata rufaa katika Mahakama ya Rufaa.

“Huu ni mchakato wa kisiasa na kisheria kwa wakati mmoja. Kwa wale wanaounga mkono BBI, wana nafasi kukata rufaa mahakamani. Kisiasa, huu ni mradi wa Rais Kenyatta na kiongozi wa ODM, Raila Odinga. Ingawa kwa wakati huu wanaonekana kupata pigo kisiasa, wao ni wanasiasa, hivyo huenda wakabuni njia mbadala kutimiza malengo yao,” Bw Kipkorir Mutai, ambaye ni mchanganuzi wa siasa.

Mnamo Ijumaa, mwenyekiti-mwenza wa Sekretariati inayoendesha mchakato huo, Bw Junet Mohamed, alisema wanaandaa kundi la mawakili ambao watakata rufaa dhidi ya uamuzi huo wiki ijayo.

Bw Mohamed, ambaye pia ni mbunge wa Suna Mashariki, alitaja uamuzi huo kama “mapinduzi ya kisheria” yanayoendeshwa na majaji wanaolenga “kulipiza kisasi” dhidi ya Rais Kenyatta.

“Uamuzi huu ni ushirikiano fiche uliopo kati ya baadhi ya maafisa wa Idara ya Mahakama na wanaharakati ili kuilemaza serikali na utendakazi wake. Ni njama zinazoendeshwa kwa ushirikiano na wanasiasa wanaoipinga serikali na juhudi za kuiunganisha nchi ambazo zinazoendelezwa na Rais Kenyatta na Bw Odinga,” akasema Bw Mohamed.

Hata hivyo, wadadisi wanaeleza kuwa licha ya baadhi ya viongozi wanaounga mchakato huo kupuuza maamuzi ya mahakama, ni hatua ambayo inaonekana kumjenga kisiasa Dkt Ruto na viongozi ambao walijitokeza wazi kuipinga BBI.

Baadhi yao ni kiongozi wa Narc-Kenya, Bi Martha Karua na Gavana Kivutha Kibwana wa Makueni.Mdadisi wa siasa Godfrey Sang’ anasema taswira ambayo imewekwa na uamuzi huo nyoyoni mwa Wakenya wengi ni kuwa Dkt Ruto ni “mtetezi wa wananchi” hata ingawa huenda hilo lisiwe kweli.

Anaeleza kuwa ingawa Dkt Ruto hakuwa amejitokeza moja kwa moja kuupinga mpango huo, kauli zake kuwa kuna masuala muhimu yanayopaswa kushughulikiwa kwanza ndiyo yanaonekana kuwateka wengi.

“Ujenzi wa dhana ni muhimu sana katika siasa. Hilo ndilo huwavutia ama kutowavutia wananchi. Ilivyo sasa, Dkt Ruto na washirika wake wanaonekana kuwa washindi kutokana na uamuzi huo, ikizingatiwa wengi wao wameadhibiwa kutokana na misimamo yao kisiasa,” akasema Dkt Sang.

Baadhi ya washirika wake waliopoteza nyadhifa zao ni Seneta Kipchumba Murkomen (Elgeyo Marakwet) kama Kiongozi wa Wengi Kwenye Seneti, Seneta Susan Kihika (Nakuru) kama Kiranja wa Wengi kwenye Seneti, Seneta Irungu Kang’ata (Murang’a) kama Kiranja wa Wengi kati ya wengine.

“Ni wazi wanasiasa hao wataonekana kama ‘mashujaa’ miongoni mwa wafuasi wao kwani wataanza kujipigia debe kwa misingi ya masaibu ya kisiasa ambayo wamekuwa wakipitia. Ni mbinu ambayo Dkt Ruto amekuwa akitumia pia, hasa kwa kutengwa serikalini na Rais Kenyatta. Bila shaka, huu ni wakati mwafaka kwao kujijenga kisiasa,” asema Dkt Sang.

Hata hivyo, wadadisi wanasema bado ni mapema, kwani hatima kamili ya uamuzi huo bado haifahamiki.“Ingawa hii ni nafasi yao kujijenga, itabidi wangoje hadi mwelekeo kamili wa mchakato huo ufahamike,” akasema.

You can share this post!

Hofu ya msambao mpya kanuniza kudhibiti corona zikipuuzwa

Mzee aliyerushwa nje ya SGR apatikana hai siku 4 baadaye