NA JAMES MURIMI
CHAMA cha Jubilee kimetangaza kuwa hakitajihusisha na misururu ya mikutano ambayo Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya umetangaza kufanya kuanzia Disemba 7.
Kinara wa Azimio la Umoja One Kenya Raila Odinga alisema mikutano hiyo ni ya kuunga mkono makamishna wanne waasi wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC).
Tayari Rais William Ruto kupitia notisi ya gazeti iliyochapishwa Ijumaa, amewatimua makamishina hao waasi kutoka IEBC na kuunda jopo la kuwachunguza ambalo litawasilisha ripoti yake kwake.
Makamishna hao ni Naibu Mwenyekiti Juliana Cherera, Francis Wanderi, Irene Masit na Justus Nyang’aya.
Jubilee inaongozwa na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ambaye pia ni mwenyekiti wa Baraza la Azimio.
Kwa mujibu wa Katibu wa Jubilee Jeremiah Kioni, hawatajihusisha na mikutano hiyo na badala yake watamakinikia jukumu lao la kupiga darubini uongozi wa Kenya Kwanza.
Hata hivyo, Bw Kioni anasisitiza kuwa wapo ndani ya muungano wa Azimio la Umoja.
“Jubilee ipo ndani ya Azimio lakini hilo halituzuii kuendelea kusukuma ajenda ya chama chetu. Tutaunga mkono serikali ambayo ipo mamlakani na pia kuikosoa kwa niaba ya Wakenya,” akasema Bw Kioni.
“Kama chama, hatuna nia ya kuendelea au kujihusisha na ghasia na hilo si sehemu ya ajenda yetu kwa sasa,” akaongeza.
Bw Odinga mnamo Jumanne alifuta mkutano wa kisiasa ambao ulikuwa unastahili kuandaliwa katika uwanja wa Kamkunji, Nairobi ili kuwaunga mkono makamishna hao wanne waasi.
Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Opiyo Wandayi alitangaza kuwa mikutano hiyo ya kisiasa iliahirishwa hadi Disemba 7 ili kupisha mitihani inayoendelea ya kitaifa ikamilike.
Katika kikao hicho cha wabunge Azimio la Umoja, Bw Wandayi alisema kuwa utawala wa Kenya Kwanza ulikuwa unalenga kulipiza kisasi, kutokana na msimamo wa makamishina hao kwa kutofautina na matokeo ya kura za Urais aliyotangaza Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati.
Kikao hicho cha wabunge wa Azimio pia kilihudhuriwa na Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, Mlezi wa chama cha DAP-K Eugene Wamalwa, Mkurugenzi wa Kanu George Wainaina na pia ulipinga hatua ya Kamati ya Sheria Bungeni kuwaagiza makamishna hao wanne wafike mbele yake.
Hivi majuzi, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Jubilee Kanini Kega alisema kuwa atawarai wakazi wa Mlima Kenya wamuunge mkono Naibu Rais Rigathi Gachagua kama kigogo wa kisiasa wa eneo hilo.
Hata hivyo, mbunge huyo wa EALA alisema atafanya hivyo akiwa ndani ya Jubilee.
“Mwanasiasa mwenye hadhi ya juu zaidi kwa sasa Mlima Kenya ni Naibu Rais Rigathi Gachagua. Watu wanafikiria tukisema kuwa tunamuunga mkono, basi tumetoka vyama vyetu ilhali mambo ni mengine,” akasema Bw Kega.
Subscribe our newsletter to stay updated