NA BRIAN OCHARO
WAATHIRIWA wa sumu ya madini katika eneo la Owino Uhuru wamepata pigo baada ya uamuzi kuhusu fidia ya Sh1.3 bilioni waliyotuzwa miaka miwili iliyopita kusukumwa mbele kwa miezi mingine mitatu.
Uamuzi huo uliokuwa ukisubiriwa kwa hamu ambao ulipangwa kutolewa jana Ijumaa ulisukumwa hadi tarehe ya baadaye kupitia mawasiliano yaliyotumwa kwa pande zinazohusika katika suala hilo.
Mahakama ya Rufaa (CoA) sasa itatoa Uamuzi huo Februari 17, 2023.Mkurugenzi mtendaji wa Kituo cha Usimamizi wa Haki na Mazingira (CJGEA) Phyllis Omido alipinga hatua hiyo akisema kuahirishwa kwa hukumu hiyo kutawaathiri zaidi waathiriwa wa sumu hiyo ambao wamekuwa wakisubiri haki kwa miaka mingi.
“Wakazi wa Owino Uhuru wamedhulumiwa wakati wote wa mchakato huu wa kutafuta haki kisheria. Wengi wamekufa na wengine zaidi wanangoja afueni kwa njia ya kupata suluhu zinazohitajika sana za kiafya,” alisema Bi Omido.
Halmashauri ya Kitaifa ya Mazingira (Nema) na Mamlaka ya Eneo la Uchakataji Mauzo ya Nje (EPZA) wamekata rufaa dhidi ya fidia ambayo itaifanya serikali kulipa mabilioni ya pesa iwapo itatupiliwa mbali.
Kuahirishwa kwa uamuzi huo kunaongeza miezi mingine ya kusubiri kwa waathiriwa wa sumu hiyo huku uamuzi huo ukitarajiwa kuathiri takriban wakazi 5000 wa jamii ya Owino Uhuru.
Mahakama ya Mazingira na Mashamba iliamuru serikali kuwalipa waathiriwa hao pesa hizo mnamo 2020 baada ya kubaini kuwa wakazi hao waliathirika kiafya kutokana na sumu hiyo.
Katika ombi lao la mwisho kwa CoA, waathiriwa waliisihi mahakama hiyo kutojitenga na maamuzi ya mahakama ya mazingira na kuiadhibu serikali kwa uzembe ulioathiri maisha yao.
Waliiomba korti kubaini kwamba mashirika ya serikali na makampuni ya kibinafsi ambayo walishtakiwa katika kesi hiyo yalipatikana yakitekeleza uchafuzi wa mazingira katika mitaa ya mabanda ambayo iliathiri afya zao.
“Nyaraka zote zilizowasilishwa mahakamani zinathibitisha kwamba Nema iliruhusu kiwanda cha EPZ Metal Refinery kufanya kazi bila kupata leseni,” waliwasilisha kupitia kwa wakili wao.
Kulingana na waathiriwa, Nema ilikuwa na taarifa kuhusu uchafuzi huo lakini ikapuuza kuchukua hatua hadi wakaazi wa mtaa huo walipoanza kukumbana na athari za uchafuzi wa mazingira uliokuwa ukifanyika eneo hilo.
“Badala ya kuchunguza na kuadhibu kampuni hiyo, Nema iliipa leseni hata baada ya kubaini kampuni hiyo imekuwa ikichafua mazingira,” walisema.
Walihitimisha kwa kudai kuwa mashirika hayo ya serikali ndio weliwezesha hatua za kampuni hizo kuchafua makazi yao kwa hivyo lazima wawajibike.
Nema ilijitetea kuwa mwaka wa 2007, sekta ya kuyeyusha betri ilikuwa tasnia mpya nchini Kenya kwa hivyo ilikuwa muhimu kuwa na majaribio ya shughuli hiyo kufanyika.
Iliendelea kusema kuwa haukuona chochote kibaya na hatua yake, na kuongeza kuwa kifungu cha 69(f) kinaiamuru kuweka mifumo ya ufuatiliaji wa mazingira na hivyo kuruhusu majaribio kufanywa.
Waathiriwa hawakuwa tu wamelipwa fidia bali serikali pia iliamriwa kusafisha eneo lililoathiriwa au kulipa faini ya Sh700 milioni.
Nema imepinga tuzo hii ikibaini kuwa CJGEA, ambayo ingedhibiti pesa hizo haina wajibu wa kikatiba au wa kisheria kuwajibikia fedha za umma.
Nema imedai kuwa kama fedha hizo zitalipwa kutakuwa na suala la uwajibikaji kuhusu fedha za umma.
“Tuzo ya Sh700 milioni haukutokana na hesabu yoyote na kwa hakika, wamepata nukuu ya Sh83 milioni kutoka kwa kampuni ya wataalamu iliyoko Kanada kwa ajili ya usafishaji huo,” Nema iliwasilisha.
EPZA ilijitenga na kesi hiyo ikibaini kuwa mamlaka ya kuamua kama mradi utakuwa na madhara kwa mazingira yako chini ya Nema.
Subscribe our newsletter to stay updated