• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 8:22 PM
Kituyi apuuzilia mbali mkutano wa Raila na OKA

Kituyi apuuzilia mbali mkutano wa Raila na OKA

Na BRIAN OJAMAA

WAZIRI wa zamani Dkt Mukhisa Kituyi amepuuzilia mbali mkutano wa hivi karibuni baina ya Rais Uhuru Kenyatta, kiongozi wa ODM Raila Odinga na viongozi wa muungano wa One Kenya Alliance (OKA).

Dkt Kituyi alitaja mkutano huo kama wa kupigania maslahi ya kibinafsi wala ‘hauna manufaa kwa Wakenya’.

Rais Kenyatta, Jumanne iliyopita alikutana na Bw Odinga na viongozi wa OKA; Gideon Moi (Kanu), Kalonzo Musyoka (Wiper), Musalia Mudavadi (ANC) na Moses Wetang’ula (Ford-K) katika Ikulu ya Mombasa.

Taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya habari na msemaji wa Ikulu, Kanze Dena, ilisema kuwa viongozi hao walijadili kuhusu janga la corona, utangamano wa kitaifa na maendeleo.Gavana wa Kakamega, Bw Wycliffe Oparanya pia alihudhuria mkutano huo.

Dkt Kituyi aliyekuwa akizungumza Jumamosi katika kijiji cha Mbakalo, eneobunge la Tongaren, Kaunti ya Bungoma katika mazishi ya Mzee Cheningi Lubao, viongozi hao hawakujadili changamoto zinazohangaisha Wakenya badala yake walizungumzia masilahi yao ya kibinafsi.

‘Kwa viongozi hao kujaribu kuungana si vibaya kwa ajili ya maendeleo ya nchi hii. Lakini sidhani kwamba muungano wao una lolote jipya litakalosaidia kukwamua taifa hili kimaendeleo,” akasema.

Waziri huyo wa zamani wa Viwanda na Biashara, alisema kuwa muungano wa viongozi hao utawazidishia wananchi maumivu badala ya kutafuta suluhisho la changamoto tele zinazowaandama.

Dkt Kituyi, aliyejiuzulu mnamo Februari kama katibu mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Biashara na Maendeleo (UNCTAD), analenga kumenyana katika kinyang’anyiro cha urais mwakani.

You can share this post!

Kingi azidi kubanwa pembeni

Bondia Okwiri apiga dafrau Fidel Munoz wa Colombia