• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Licha ya kupata makamishna 7, IEBC bado inayumba

Licha ya kupata makamishna 7, IEBC bado inayumba

Na LEONARD ONYANGO

HUKU ikiwa imesalia chini ya miezi 11 kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9, 2021, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ingali inakabiliwa na masaibu tele.

Utata kuhusu kandarasi ya vifaa vya kielektroniki vya kusajili na kutambua wapigakura, uhaba wa wafanyakazi, marekebisho ya baadhi ya sheria zinazohusiana na uchaguzi na sintofahamu kuhusu usajili wa wapigakura, bado ni changamoto kubwa zinazokumba IEBC.

Wito wa kumtaka mwenyekiti wa tume hiyo Bw Wafula Chebukati ajiuzulu kutoka kwa baadhi ya viongozi wa chama cha ODM pia huenda ukatatiza maandalizi ya uchaguzi.

Viongozi wa ODM, wakiongozwa na mwenyekiti wao John Mbadi wanataka Bw Chebukati asisimamie uchaguzi mkuu ujao huku wakidai kwamba Wakenya wamepoteza imani naye.

Viongozi wa ODM wamekuwa wakidai kuwa mwenyekiti wa IEBC anaegemea upande wa Naibu wa Rais William Ruto – madai ambayo Bw Chebukati ameyakanusha vikali.

Tayari IEBC imevuka kizingiti cha kwanza baada ya makamishna wanne; Juliana Cherera, Francis Wanderi, Irene Masit na Justus Nyang’aya kuapishwa Alhamisi kujaza nafasi zilizoachwa wazi na Roslyne Akombe, Nkatha Maina, Margaret Mwachanya na Paul Kurgat waliojiuzulu miaka mitatu iliyopita.Tangu 2018, IEBC imekuwa ikiendeshwa na Bw Chebukati, Abdi Guliye na Boya Molu.

Uamuzi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa kwamba IEBC inahitaji kuwa na angalau kuwa na makamishna watano kuendesha shughuli zake zinazohusiana na sera ulizua hofu kwamba baadhi ya maandalizi ya uchaguzi yaliyofanywa na watatu hao huenda yakafutiliwa mbali.

Bodi ya Kukagua Zabuni za Umma (PPARB) Alhmisi ilifutilia mbali mchakato wa utoaji wa kandarasi ya ununuzi wa vifaa vya kielektroniki vya kusajili na kutambua wapigakura na kupeperusha matokeo (KIEMS).

SHERIA

Bodi ya PPARB ilisema kuwa IEBC haikufuata sheria katika kutangaza zabuni hiyo mnamo Aprili, mwaka huu.Mnamo Agosti 11, mwaka huu, Risk Africa Innovatis Ltd –ambayo ni kampuni ya Kenya – ilishtaki IEBC kwa bodi ya PPARB ikisema kuwa tume hiyo ilikiuka sheria kwa kufungia nje kampuni za humu nchini.

PPARB iliagiza IEBC kutangaza upya kandarasi hiyo ndani ya siku 45 zijazo. Hiyo inamaanisha kwamba shughuli ya utoaji wa kandarasi ya vifaa vya KIEMS huenda ikajikokota hadi Novemba, mwaka huu.

IEBC pia inakabiliwa na shinikizo za kuitaka kutotumia KIEMS za kampuni ya Idemia Securities Ltd (ambayo awali ilifahamika kama OT Morpho) iliyotumiwa 2017 lakini ikafeli siku ya uchaguzi. IEBC inahitaji tableti 55,000 za kusajili na kutambua wapigakura na kupeperusha matokeo katika vituo 53,000 kote nchini.

Mwanakandarasi atakayepewa zabuni hiyo pia atahitajika kununua mtambo wa kuhifadhi taarifa za wapigakura (sava).Sava ya sasa ina uwezo wa kuhifadhi taarifa za wapigakura milioni 20 tu.IEBC inalenga kusajili wapigakura wapya milioni 6 mwishoni mwa mwaka huu.

Kujikokota kwa kandarasi hiyo kunamaanisha kuwa huenda shughuli ya kusajili wapigakura wapya ikafanyika kati ya Januari na Machi mwaka ujao.IEBC tayari imetangaza nafasi 7,540 za makarani wa usajili wa wapigakura, wasimamizi 1,450 na wataalamu wa Teknolojia ya Mawasiliano (ICT) 580.

Makataa ya kutuma maombi yalikamilika Agosti 27, mwaka huu, na makarani wa muda watakaoajiriwa kwa muda, watalazimika kungojea kwa miezi kadhaa kabla ya kuanza kazi.Kulingana na mwongozo wa utendakazi wa 2020-2024, IEBC inakumbwa na uhaba wa wafanyakazi wa kudumu 290.

Kwa mfano, katika idara ya ICT ambayo hushughulika na masuala ya kidijitali, usalama wa sava ya wapigakura, kupeperusha matokeo na masuala ya intaneti, kuna uhaba wa wafanyakazi 13.

Wafanyakazi hao wapya wanahitaji kuajiriwa mapema ili kupata muda wa kutosha kupewa mafunzo kuhusiana na vifaa vipya vya KIEMS vitakavyonunuliwa.Tume ya IEBC pia ilipanga kushawishi Bunge kufanyia marekebisho sheria sita zinazohusiana na uchaguzi kabla ya Agosti 2022.

Miongoni mwa sheria inayolengwa kufanyiwa marekebisho kabla ya uchaguzi wa Agosti 9, 2022 ni Sheria ya Matumizi ya ICT katika uchaguzi ambayo tume inasema kuwa sheria ya sasa inakanganya.

Sheria nyingine ambayo IEBC iko mbioni kuhakikisha kuwa inarekebishwa ni kuhusu usajili wa wapigakura katika mataifa ya kigeni.

IEBC inasema ukosefu wa takwimu kuhusu idadi ya halisi ya Wakenya walio katika kila nchi ni changamoto kubwa katika usajili wa wapigakura walio ughaibuni.

Idadi ya Wakenya wanaoishi ughaibuni walio katika daftari la wapigakura ni 4,224, kwa mujibu wa IEBC.

You can share this post!

DINI: Kila dakika unapokuwa na hasira, unapoteza sekunde...

BBI: Huenda juhudi za bunge zisizae matunda