• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:50 AM
Mshirika wa karibu wa Shahbal ahamia UDA

Mshirika wa karibu wa Shahbal ahamia UDA

NA MWANDISHI WETU

Mwaniaji wa kiti cha Uwakilishi wa Wanawake Kaunti ya Mombasa Bi Miraj Abdullahi sasa ameachana na mshirika wake mkubwa Suleiman Shahbal wa ODM na kuingia chama cha UDA. Mshirika wake mkuu sasa ni aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar.

Akiongea na wanahabari mjini Mombasa, Bi Miraj alisema kuwa hatafanya kazi na Shahbal kwani ameamua kuendeleza ajenda yake ya kisiasa kupitia kwa chama cha UDA kinachohusishwa na Dkt Ruto.

“Sitashirikiana tena na Bw Shahbal licha ya kwamba tumekuwa pamoja kwa muda wa miaka kumi iliyopita. Wakati umefika kwangu kuendeleza ajenda yangu ya kisiasa ambayo inaonekana kwamba haiungi mkono,” Bi Miraj akasema.

Alifichua kuwa ndoto yake ya kuwania kiti cha Mbunge Mwakilishi wa Mombasa ndiyo ilivuruga uhusiano wake na Bw Shahbal.

“Urafiki kati yetu unapaswa kuruhusu kila mmoja wetu kujiendeleza. Tunapaswa kuendeleza ndoto zetu. Bw Shahbal hajakuwa akiunga mkono ndoto yangu ya kisiasa tangu tulipokutana mnamo 2013,” Bi Miraj akasema.

Bi Miraj aliandikisha historia kwa kuwa mwaniaji wa kike mwenye umri mdogo zaidi kuwania wadhifa wa udiwani katika Wadi ya Tononoka, Mombasa katika uchaguzi mkuu wa 2013.

Aliwarai wakazi wa Mombasa kuunga mkono ndoto yake ya kisiasa anapojiandaa kuwania kiti cha Mbunge Mwakilishi wa Wanawake.

Lakini katika ujumbe alioweka kwenye ukurasa wake wa Facebook Shahbal alisema hataruhusu tofauti za kisiasa kuvuruga uhusiano wao.

“Nimemjua Miraj kwa zaidi ya miaka 10. Naheshimu uamuzi wake wa kujiunga na UDA kwa sababu ni wito kutoka katika nafsi yake. Sitaruhusu urafiki wetu wa miaka 10 kuharibiwa na tofauti zetu za kisiasa,” akasema.

“Nawaomba wafuasi wangu wasimharibie sifa kupitia mitandao ya kijamii. Kazi yake katika mradi wa Buxton Point ni tofauti na haitaingiliana hata kidogo na azma yake,” Bw Shahbal alisema katika ujumbe wake.

Hata hivyo, Bi Miraj alitangaza kujiuzulu kutoka wadhifa wake kama Mshirikishi wa Mradi wa Buxton Point.

You can share this post!

Sahib asherehekea ‘bathdei’ kwa kutawala Autocross...

Viongozi Mlima Kenya watazuru Nyanza kuthibitisha wanaunga...