NA MWANDISHI WETU
RAIS William Ruto ameonekana kutekeleza kimya kimya mapendekezo ya Jopo la Maridhiano (BBI), ambayo alikuwa mstari wa mbele kuyapinga.
Katika kile kinachoonekana kuwa utekelezaji wa mapendekezo hayo, Rais Ruto aliendeleza kampeni zinazozingatia sera badala ya masuala ya kugawanya wananchi kwa misingi ya kikabila kati ya mengine.
Kuendeleza kampeni kwa kutumia sera ya uchumi wa kuinua Mkenya wa tabaka la chini, maarufu ‘Bottom Up,’ Dkt Ruto alibadili jinsi ambavyo Wakenya walikuwa wamezoea siasa.
Jambo hili ni kati ya mapendekezo ya BBi kuhusu Sura ya Saba ya Katiba.
Waasisi wa BBI walitaka marekebisho kuhusu Uwakilishi wa Watu, ili kuhimiza mashindano ya kisiasa kwa misingi ya sera, fikira na maadili, badala ya siasa ambapo kila baada ya uchaguzi watu hutengana.
Kwa mara ya kwanza kwa miaka mingi, Wakenya walimaliza uchaguzi na kila mmoja akaendelea na shughuli zake, bila ya polisi kufyatua hata kitoa machozi kimoja.
BBI ilipendekeza kwamba, Sura ya Nane ya Katiba ifanyiwe marekebisho, ili serikali iwe ndani ya Bunge.
Waliotoa mapendezo kwa jopo lililoongozwa na aliyekuwa Seneta wa Garissa, marehemu Mohamed Yussuf Haji walitaka mawaziri wawe wakiitwa bungeni kujibu maswali na kufafanua sera zao.
Punde tu baada ya kuapishwa, Dkt Ruto alitangaza kwamba, anapanga kutoa agizo rasmi la kuwawezesha mawaziri kuhudhuria vikao vya bunge na kujibu maswali pamoja na kueleza sera za serikali.
“Nitatoa agizo la kurekebisha kanuni za Bunge, kuhakikisha mawaziri wa serikali yangu watakuwa wakifika bungeni,” akasema katika uwanja wa michezo wa Moi, Kasarani.
Pendekezo jingine la BBI ambalo tayari Dkt Ruto amelitekeleza ni lile la kuirekebisha Sura ya Tisa ili kupanua Serikali pamoja na kuunda wadhifa wa Waziri Mkuu.
Wiki jana alipotangaza Baraza lake la Mawaziri, Dkt Ruto alitaja idara saba za ziada katika wizara hizo, ikilinganishwa na sasa ambapo kuna idara 42 pekee.
Kadhalika, alimtaja Kinara wa chama cha Amani National Congress (ANC) Musalia Mudavadi kuwa Waziri Mkuu.
Ingawa wadadisi wamekuwa wakitaja wadhifa huo kuwa usiokuwa na mamlaka, kubuniwa kwake pekee kunatimiza ndoto ya Wakenya kuwa na Waziri Mkuu.
Inatarajiwa pia kuwa Bw Mudavadi atakuwa akifanya kazi yake Bungeni, akiwa kiongozi wa sera za Serikali katika jumba hilo la kutunga sheria.
“Waziri Mkuu atakuwa Musalia Mudavadi. Ni wadhifa wa tatu kwa ukubwa baada ya Rais na Naibu Rais. Nimeandaa majukumu ya ofisi hiyo. Atamsaidia Rais na Naibu Rais katika kushirikisha miradi ya serikali na kusimamia shughuli za serikali katika wizara zote,” alisema Dkt Ruto alipokuwa akimteua.
Walipotoa maoni kuhusu BBI, Wakenya pia walitaka kifungu cha 77 (1) kibadilishwe ili mawaziri wawe wanatoka bungeni.
Ingawa hili hajalitekeleza kikamilifu, Dkt Ruto amewachomoa wabunge kadhaa na kuwapa nyadhifa za uwaziri.
Wabunge Aden Duale (Garissa Mjini), Alice Wahome (Kandara) na Seneta wa Elgeyo Marakwet sasa wanasubiri Bunge kuwaidhinisha kuwa mawaziri.
Seneta wa Bungoma (Moses Wetangula) pia alipewa uspika katika Bunge la Kitaifa.
Mojawapo ya mapendezo ya mwisho ya BBI ni kuhusu usimamizi wa pesa. Alipokuwa akihutubu baada ya kula kiapo, Rais Ruto aliamuru bajeti ya Inspekta Jenerali wa Polisi iondolewe kutoka Afisi ya Rais. Amri hiyo ilitekelezwa siku iliyofuata.
Subscribe our newsletter to stay updated