• Nairobi
  • Last Updated May 20th, 2024 9:16 PM
Ruto, Muturi wasuta mabwanyenye wa MKF kwa kudai ndio wenye ufunguo wa kura za Mlima Kenya

Ruto, Muturi wasuta mabwanyenye wa MKF kwa kudai ndio wenye ufunguo wa kura za Mlima Kenya

Na SAMMY WAWERU

SIKU mbili baada ya wakfu wa wafanyabiashara kutoka Mlima Kenya – Mount Kenya Foundation (MKF) – kukutana na vinara wa One Kenya Alliance (OKA), baadhi ya viongozi na wanasiasa wamejitokeza na kukashifu kauli ya mabwanyenye wa muungano huo kwamba “wao ndio wenye ushawishi na maamuzi ya kura za eneo la Kati”.

MKF ikiongozwa na mwenyekiti wake, Bw Peter Munga na naibu, Titus Ibui, Alhamisi ilifanya kikao na Mabw Musalia Mudavadi (ANC), Kalonzo Musyoka (Wiper), Moses Wetang’ula (Ford-Kenya) na Gideon Moi (Kanu), katika mkahawa wa kifahari wa Safari Park, jijini Nairobi, na kuahidi itajua mgombea itakayeunga mkono 2022 kuwania urais.

Aidha, MKF ilisema itatathmini manifesto ya kila mwaniaji na kufanya maamuzi ya nani itaunga.

Wakfu huo wiki iliyopita pia ulikutana na kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga.

Kufuatia mikutano hiyo, baadhi ya viongozi na wanasiasa wamejitokeza na kukashifu MKF wakisema haina ufunguo wa kura za jamii ya Mlima Kenya.

Wakiongozwa na naibu wa rais, Dkt William Ruto, wamesema Wakenya ndio wana kura ila si “mabwanyenye wachache wanaokongamana hotelini kwa sababu zao za kibinafsi”.

“Ni wao wataamua au ni nyinyi Wakenya wenye kura?” Bw Ruto akataka kujua akihutubia umati wa watu Laikipia mnamo Jumamosi.

Naibu wa rais ni kati ya wanasiasa ambao wametangaza nia yao kuwania urais mwaka ujao.

Naye Spika wa Bunge la Kitaifa, Bw Justin Muturi akionekana kusuta MKF alisema wanaomezea mate kiti cha urais wanapaswa kujituma mashinani ili kujua mahitaji ya wananchi.

“Mkikaa hotelini na kupanga urithi wa serikali mtajuaje mahitaji ya Wakenya? Acheni wananchi wajiamulie wanayetaka awaongoze,” Bw Muturi akasema.

Spika huyo pia ametangaza kuwa debeni, katika kinyang’anyiro kumrithi Rais Uhuru Kenyatta 2022.

Wakfu wa wafanyabiashara kutoka Mlima Kenya unajumuisha wafanyabiashara tajika na wenye ushawishi mkuu eneo la Kati na nchini kiuchumi.

You can share this post!

Karugu ataka madiwani wazuiwe kumtimua ofisini

Maafisa watatu wakuu wa polisi kujua hatma yao octoba 28