NA COLLINS OMULO
NAIBU Rais Dkt William Ruto wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) ndani ya muungano wa Kenya Kwanza amemteua Mbunge wa Mathira Rigathi Gachagua awe mgombea mwenza wake kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022.
Akifichua jina la mgombea mwenza wake Jumapili, Dkt Ruto amesema muungano wa Kenya Kwanza umeoanisha ajenda mbalimbali za vyama washirika ili kuendana na mpango wa kiuchumi wa Kenya Kwanza katika mkutano uliodumu saa 17.
Mnamo Jumamosi kulikuwa na vuta nikuvute katika makazi ya Dkt Ruto mtaani Karen alipotarajiwa kumtangaza mgombea mwenza wake.
Wakati huo ilitarajiwa ama angemchukua Seneta wa Tharaka Nithi Profesa Kithure Kindiki au Bw Gachagua.
Kindiki hakuhudhuria hafla hiyo. Hata hivyo Dkt Ruto amemsifu Profesa Kindiki, akimtaja kama “wakili wangu na rafiki.”
“Ingawa hayuko hapa, rafiki yangu Abraham Kithure Kindiki aliyeibuka wa pili alileta msisimko wa aina yake katika mbio hizi,” Dkt Ruto amesema.