• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 4:40 PM
Uhuru amtembeza Raila jijini usiku

Uhuru amtembeza Raila jijini usiku

Na BENSON MATHEKA

Yaonekana Jumatatu ilikuwa siku ya Rais Uhuru Kenyatta kuyafurahisha makundi mawili hasimu ya kisiasa yanayounga mkono kinara wa ODM Raila Odinga na Naibu Rais William Ruto.

Mchana baada ya kushiriki maadhimisho ya Sikukuu ya Madaraka ambapo alitagusana na naibu wake, Dkt Ruto kwa bashasha na uchangamfu, usiku ilikuwa zamu ya Rais kumtembeza Bw Raila kwenye gari lake jijini Nairobi.

Rais Uhuru na waziri huyo mkuu wa zamani waliwagutusha Wakenya walipoamua kutembelea barabara za jiji la Nairobi usiku wakati wa kafyu.

Ziara hiyo iligunduliwa baada ya video iliyonaswa na kamera za usalama kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii.

Kwenye video hiyo, gari moja linaonekana likisimama kwenye barabara ya Kenyatta Avenue kabla ya Rais Kenyatta kushuka kutoka kiti cha dereva na kufuatwa na Bw Odinga anayeshuka kiti cha mbele kando ya dereva.

Bw Odinga anaungana naye kando ya barabara huku maafisa kadhaa wa kikosi cha ulinzi wa rais wakikaa chonjo kuhakikisha usalama.

Magari mengine mawili yanayoaminika kuwa ya walinzi wa rais yanafika na kusimama nyuma ya gari ambalo viongozi hao wawili walishuka.

Video hiyo pia inaonyesha afisa wa usalama aliyejihami kwa bunduki akishika doria kwenye barabara hiyo.

Viongozi hao wawili wanaonekana wakitembea kwa miguu ishara kwamba huenda walikuwa wakikagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Shirika la Huduma la jiji la Nairobi na viunga vyake (NMS) ambalo Rais Kenyatta alibuni kufuatia mkataba wake na Gavana Mike Sonko wa kuhamisha majukumu hadi serikali ya kitaifa.

Wawili hao wanaonekana wakitembea huku magari hayo yakiwafuata. Ziara hiyo pia ilimpa Rais fursa ya kubaini iwapo marufuku ya kutotoka nje usiku yalikuwa yakitekelezwa jijini.

Ingawa video hiyo haionyeshi tarehe iliyonaswa, inaaminika kuwa ilikuwa Jumatatu usiku baada ya sherehe za Madaraka Dei zilizofanyika ikulu ya Nairobi.

Kuonekana kwao pamoja katika barabara za Nairobi kunaonyesha ukuruba wao tangu handisheki yao ya Machi 9 2019, umeendelea kuimarika. Kabla ya kufika barabara ya Kenyatta Avenue, wawili hao walikuwa wametembelea sehemu kadhaa za katikati mwa jiji.

Baadhi ya walinzi walisema waliona msafara wa magari matatu katika barabara ya Waiyaki.

Walinzi wa usiku katika barabara za jiji ambao hawakutaka majina yao yachapishwe walisema wawili hao walionekana wachangamfu wakikagua hata mitaro ya maji taka na taa za barabarani.

Rais Kenyatta amekuwa akifanya ziara za ghafla kukagua miradi ya maendeleo lakini hajawahi kuonekana na Bw Odinga katika barabara za Nairobi usiku.

Amewahi kutembelea Kaunti ya Nyeri kukagua ukarabati wa reli na akatembelea uwanja wa Nyayo kukagua maandalizi ya uwanja huo wakati wa ibada ya wafu ya hayati Daniel Moi.

Aliwahi kuzuru bandari ya Kisumu akiwa na Bw Odinga bila kutarajiwa.

Mapema siku hiyo, kiongozi huyo wa nchi alikuwa pamoja na Naibu Rais katika sherehe za Madaraka, hali iyozua furaha miongoni mwa wafuasi wa Dkt Ruto waliodhani Uhuru alikuwa na mpango wa kumsaliti mdogo wake serikalini.

Hata hivyo, matukio hayo mawili yanashadidia kauli ya Rais kuwa nia yake ni kuunganisha taifa badala ya kuligawanya.

You can share this post!

Afueni kwa wafanyabiashara wa Mombasa

Vita vya Ford Kenya vyatua kwa Msajili wa Vyama

adminleo