• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Wafuasi 13 wa UDA washtakiwa kwa ukiukaji wa kanuni za corona

Wafuasi 13 wa UDA washtakiwa kwa ukiukaji wa kanuni za corona

Na George Odiwuor

WAFUASI 13 wa chama cha UDA katika Kaunti ya Homa Bay, Jumatatu walipigwa faini ya Sh2,000 kila mmoja kwa kukiuka masharti ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona.

Wafuasi hao walikamatwa Ijumaa iliyopita walipokuwa kwenye mkutano katika mkahawa mmoja mjini Homa Bay.Hata hivyo, walilalamika dhidi ya kubaguliwa.

Watu hao walifikishwa mbele ya Hakimu Mkuu wa Homa Bay, Joy Wesonga, Jumatatu, ambapo walikubali makosa yao.Walishtakiwa kwa kushiriki kwenye mkutano kinyume na kanuni zilizowekwa na serikali.

Viongozi wa chama hicho walilipa faini hizo ijapokuwa walilalamikia “maonevu” dhidi yao na polisi. Viongozi hao walijumuisha mwanaharakati George Ayudi na Mshirikishi wa UDA katika eneo la Nyanza, Bw John Waria.

“Polisi hawapaswi kutumika na wanasiasa. Tuko katika nchi huru ambapo kila mmoja ana haki kujiunga na chama chochote cha kisiasa,” akasema. Aliongeza kuwa washiriki walihakikisha hawakuwa wamekaribiana, kama inavyohitajika na Wizara ya Afya.

Alisema walikuwa wamezingatia masharti hayo yote.Wanaharakati wa kisiasa katika eneo hilo pia walikashifu mtindo wa polisi kuwakamata watu kila mara kwa kisingizio cha kukiuka masharti hayo.

Walisema Mahakama Kuu tayari imefutilia mbali masharti hayo, hivyo watu wako huru kushiriki kwenye mikutano ya kisiasa.

You can share this post!

Polisi mpakani wapepeta corona kwa hongo ya Sh2,000

Manusura wa jengo lililoporomoka aaga dunia