KASSIM ADINASI NA PIUS MAUNDU
WANASIASA waliomuasi kiongozi wa ODM, Raila Odinga, baada ya kushindwa kwenye uchaguzi mkuu wa Agosti 9 sasa wameanza kubuni safari mpya za kisiasa.
Hii ni baada ya baadhi yao kukosa kuteuliwa katika nyadhifa tofauti katika serikali ya Kenya Kwanza.
Wanasiasa kadhaa walikuwa wakitarajia kuokolewa kisiasa na Rais William Ruto baada ya kumfanyia kampeni katika eneo la Nyanza, ambalo ni ngome ya kisiasa ya Bw Odinga.
Hata hivyo, mikakati ya baadhi yao haikuenda vile walivyopanga, ambapo sasa wanamrai Rais Ruto kuwarejeshea mkono kutokana na mchango waliotoa kwenye kampeni hizo.
Akihutubu kwenye hafla iliyohudhuriwa na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia (ICT), Eliud Owalo, mbunge Jared Okello (Nyando) aliuomba utawala wa Kenya Kwanza kuwapa kazi wanasiasa kutoka eneo hilo walioshindwa kwenye nyadhifa tofauti waliowania kwenye uchaguzi huo kwa kumfanyia kampeni Dkt Ruto.
Bw Owalo alikuwa akitoa chakula cha msaada kwa jamii tofauti katika eneo hilo.
Akasema Bw Okello: “Wanasiasa hao wanafaa kuteuliwa kuhudumu katika baadhi ya nafasi serikalini ili kutoanza kuipinga serikali. Ni watoto wetu waliofanya kazi vizuri sana. Hawapaswi kuachwa kwenye baridi.”
Baadhi ya wanasiasa walihamia katika Kenya Kwanza baada ya uchaguzi huo, hali inayoonekana kudidimiza uwezekano wa wanasiasa hao kuteuliwa serikalini.
Wanasiasa hao wanajumuisha aliyekuwa Gavana wa Nairobi, Evans Kidero, aliyekuwa Seneta wa Kisumu Fred Outa, wabunge wa zamani Nicholas Gumbo (Rarieda), Edick Anyanga (Nyatike), Martin Ogindo (Rangwe) na Olago Aluoch (Kisumu Magharibi).
Aliyekuwa gavana wa Migori Okoth Obado na Jack Ranguma (Kisumu) ni miongoni mwa wanasiasa walioasi wimbi la Azimio katika eneo hilo kwa kumpigia debe Rais Ruto.
Wanasiasa waliojaribu kuwania tena ubunge bila mafanikio ni Martin Ogindo (Rangwe), Edick Anyanga (Nyatike), Nicholas Gumbo (Rarieda), Bw George Omondi Muluan (Alego Usonga), Bw Joseph Ndiege (Suna Magharibi), Neto Oyugi (Ndhiwa) na George Oner (Rangwe).
Wale waliopoteza nyadhifa zao kwenye uchaguzi huo wamekuwa wakitarajia kuteuliwa kuhudumu katika nyadhifa tofauti serikalini ili kutodidimia kisiasa.
Kwa miongo miwili iliyopita, wapigakura katika eneo la Nyanza wamekuwa wakikataa kuwachagua viongozi wanaojaribu kurejea katika ulingo wa kisiasa baada ya kushindwa kwenye chaguzi za awali.
WACHACHE
Haya hivyo, kuna wachache ambao wamehimili ghadhabu za wapigakura.
Mnamo 1997, aliyekuwa mbunge wa Alego Usonga, Oloo Aringo, alifanikiwa kushinda tena ubunge baada ya kushindwa na mwanahabari wa zamani Otieno Mak’Onyango.
Gavana Ochilo Ayacko wa Migori alifanikiwa kurejea siasani, baada ya kukaa miaka kumi kwenye baridi ya kisiasa.
Alipoteza kiti chake cha ubunge cha Rongo baada ya kushindwa na Dalmas Otieno kwenye uchaguzi wa 2007.
Katika eneo la Ukambani, wanasiasa waliohamia katika Kenya Kwanza kutoka Azimio wanangoja kuona ikiwa watateuliwa kwenye nyadhifa kuu serikalini hata baada ya Rais Ruto kuwateua mawaziri.
Wanasiasa hao ni aliyekuwa Seneta wa Kitui, David Musila, aliyekuwa gavana wa Makueni Kivutha Kibwana na aliyekuwa naibu wake, Bi Adelina Mwau.
Bw Musila na Prof Kibwana wamekuwa wakijaribu kuwaleta pamoja washirika wa Dkt Ruto katika eneo hilo.
Anasema eneo hilo halitakubali kubaki katika upinzani kwa muhula mwingine.
Subscribe our newsletter to stay updated