• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:55 AM
Bandari FC iko tayari kuishinda Equity FC mechi ya nusu fainali

Bandari FC iko tayari kuishinda Equity FC mechi ya nusu fainali

Na ABDULRAHMAN SHERIFF

BANDARI FC imepania kuhakikisha inahifadhi taji lao la FKF Betway Cup itakapokutana na  Equity FC kwenye mechi ya robo fainali itakayochezwa uwanja wa Utalii jijini Nairobi kesho Jumatano.

Bandari, timu ya pekee kutoka jimbo la Pwani kushiriki Ligi Kuu ya Kenya na ambayo iliwahi kushiriki kwenye dimba la Caf Confederation Cup ilifanikiwa kujiandikishia nafasi ya robo fainali baada ya kuinyuka Sagalagala TTI kwa mabao 5-0 juzi Jumapili.

Kocha Andre Cassa Mbungo amesema amefurahikia mno na jinsi vijana wake walivyocheza kwa uelewano na kupata ushindi mkubwa zaidi ya ule walioupata kwenye mechi ya raundi ya timu 32 ilipoilaza Dimba Patriots kwa mabao 5-1.

“Nina imani kubwa tutapata ushindi kwenye mechi yetu ya robo fainali dhidi ya Equity FC hapo Jumatano. Tunataka tufuzu kwa nusu fainali kwani tutakuwa tumebakisha kushinda mechi mbili pekee tuweze kuhifadhi taji letu,” akasema Mbungo.

Mkufunzi huyo anasema wana hamu kubwa ya kushiriki kwenye dimba la Caf Confederation Cup ili tuweze kuiwakilisha Kenya kwenye mashindano hayo ya barani Afrika. “Hivyo, nina uhakika vijana wangu watafanya bidii zaidi waweze kushinda mechi tatu tuweze kuwa  mabingwa tena,” akasem a.

Kocha Mbungo anasema kuwa hakuna mchezaji yoyote yule aliyepata majeraha wakati wa mechi yao na Sigalagala na hivyo, atakuwa na kikosi kamili wakati watakapokipiga na Equity hapo kesho.

Katika mchezo wao wa raundi ya timu 16 dhidi ya Sagalagala, Benjamin Mosha alitinga mawili dakika tatu na 39, Wilberforce Lugogo akafunga dakika ya 18, Yema Mwana akatinga lake dakika ya 49 na beki wa Sigalagala akajifunga la tano dakika ya 90.

Wakati huo huo, meneja wa Bandari FC Albert Ogari amesema kuwa winga wao Shaaban Kenga aliyevunjika mguu miezi kadhaa zilizopita, ameanza mazoezi mepesi. “Tunatarajia kwa kipindi kifupi kijacho, Kenga atajumuika na wanasoka wenzake kwa mazoezi ya pamoja,” akasema.

  • Tags

You can share this post!

KRU kuleta mastaa wa Kenya Simbas mechi za kuingia Kombe la...

Zamu ya Safari Rally kumulikwa baada ya Ogier kushinda...