• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
‘Ni kibarua kigumu kumsaidia Miguna’

‘Ni kibarua kigumu kumsaidia Miguna’

CHARLES WASONGA na JUSTUS OCHIENG’

MAWAKILI, watetezi wa haki za kibinadamu na baadhi ya wanasiasa wameelezea kutamaushwa kwao na msimamo mkali wa mwanaharakati wa upinzani Miguna Miguna ambao wanadai, unatatiza jitihada za kumsaidia dhidi ya ukandamizaji wa Serikali.

Japo Wakenya wengi wamejitokeza kumtetea Dkt Miguna, wakili huyo amejitokeza kama mkaidi na muasi hata kwa wale wanaoendelea kumsaidia kurejea nchini kama raia wa Kenya.

Licha ya kinara wa upinzani Raila Odinga na chama cha ODM kuweka juhudi za kumkomboa Dkt Miguna, jana wakili huyo anayeendelea kuzuiliwa nchini Dubai, alimkemea vikali Bw Odinga na kumshutumu kwa kushirikiana na wanaomkandamiza.

Katika uwanja wa ndege wa JKIA ambapo sarakasi zilianzia Jumatatu, Bw Odinga alijaribu kumshawishi Dkt Miguna ashirikiane na maafisa wa idara ya uhamiaji katika uwanja wa ndege wa JKIA ili aruhusiwe kuingia nchini lakini akakataa.

Bw Odinga alionekana akipiga simu kila mara kuashiria alikuwa akiwasiliana na viongozi wakuu serikalini, akiwemo, Rais Uhuru Kenyatta ili kumsaidia Miguna.

Jumamosi, chama cha ODM kilisema kimekuwa kikitoa huduma za mawakili kwa Dkt Miguna bila malipo kwa maagizo ya Bw Odinga.

“Tumeorodhesha juhudi zote ambazo kiongozi wa chama chetu zinazolenga kumsaidia Dkt Miguna. Mzee (Raila) amewaamuru mawakili wake wote, nikiwemo mimi kushughulikia kesi ya Miguna.

Mawakili hao, wakiongozwa na Orengo wamekuwa wakishughulikia kesi yake tangu Februari alipokamatwa,” akasema Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna.

Akaongeza: “Tumedhulumiwa na polisi na maafisa wa serikali kiasi cha paspoti zetu kutwaliwa. Mzee amekuwa akihudhuria vikao vya kesi hiyo mahakamani.

Na alikuwa katika uwanja wa ndege akihatarisha usalama akishughulikia kesi hiyo. Kwa hivyo, madai kwamba Mzee amemtelekeza Dkt Miguna hayana msingi.”

Jumamosi, Dkt Miguna alimsuta Bw Odinga kwa kumtelekeza na kutofanya lolote kumsaidia na kuendelea kushirikiana na “watu ambao walimwibia kura na kuwaua wafuasi wake baada ya uchaguzi wa mwaka jana”.

Lakini Bw Sifuna na wabunge; Opiyo Wandayi (Ugunja), Samuel Atandi (Alega Usonga) na Gideon Ochanda (Bondo) walimwonya Miguna dhidi ya kumshambulia Bw Odinga kuhusu masaibu yake.

 

Kumshambulia Raila

“Raila Odinga ni taasisi, hafai kushutumiwa. Yeye na Raila hawachezi katika ligi moja. Miguna anavuka mstari mwekundi sasa kwa kumshambulia Odinga,” akasema Wandayi ambaye pia ni Katibu wa Masuala ya Kisiasa katika ODM.

Dkt Miguna ambaye aliwasili kutoka Canada Jumatatu alitakiwa kujaza fumo maalum ili apewe viza ya miezi sita lakini akakataa licha ya kudinda kuwasilisha paspoti yake ya Canada.

Licha ya wanahabari kujeruhiwa vibaya na maafisa wa polisi waliofika JKIA kufuatilia masaibu ya Dkt Miguna mapema wiki hii, wakili huyo aliwashambulia wanahabari vikali akidai wameshawishiwa na serikali ya Jubilee ili kupuuza habari kumhusu.

“Nimefanyiwa mahojiano na vituo vya BBC, VOA na Radio France International na hakuna mwanahabari wa Kenya amenihoji hata kupitia kwa simu..wanaendelea kuchapisha tu uwongo kunihusu,” alisema Dkt Miguna licha ya habari zake kupewa kipaumbele katika magezeti, runinga na redio za humu kwa kipindi cha wiki moja sasa.

Duru zinasema ubalozi wa Canada umekuwa na wakati mgumu kumsaidia Dkt Miguna kutokana na misimamo yako mikali.

Kwenye kanda za video zilizonaswa katika uwanja wa JKIA, ilidhihirika kuwa Dkt Miguna alijibizana vikali na mawakili wake. Anasikika akiwafokea walipopendekeza atie saini stakabadhi ambazo zingemruhusu kupewa viza ya kuingia nchini.

 

Kurarua stakabadhi

Alitwaa stakabadhi hizo na kuzirarua akidai maafisa wa idara ya uhamiaji walipaswa kumruhusu aingie nchini bila masharti yoyote.

Mmoja wa mawakili wa Miguna Bi Judy Soweto anakiri mteja wake ni “mtu mgumu’ nyakati nyingine.

“Ni kweli kwamba mara nyingi Miguna hujitokeza kama mtu asiyekubali kulegeza msimamo, ni mkakamavu na mkaidi lakini madai mengine anayowekelewa sio kweli,” akasema Bi Soweto.

Wakili huyo alisema hayo kujibu madai ya Mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNHRC) Kagwiria Mbogori aliyemtaja Miguna kama mkaidi aliyedinda kushirikiana na maafisa wa serikali waliotaka kumsaidia.

“Nimetamaushwa na Miguna kwa sababu agizo la mahakama lilimruhusu kutumia paspoti yake ya Canada kuingia humu nchini. Lakini alikataa katakata kuwasilisha stakabadhi hizo za usafiri kusudi aruhusiwe kuingia nchini,” akasema Bi Mbogori.

Wakili Miguna pia alikana watu wa familia yake, wakiongozwa na kakake Eric Ondiek, waliotoa wito kwa jamii ya kimataifa kuingilia kati kumnusuru. Alisema msemaji wake ni “mke wangu anayeishi Canada na sitambui mtu mwingine.”

You can share this post!

Joho amtembelea Miguna hospitalini Dubai

Trump atarajiwa kuzuru Kenya

adminleo