• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Wasiwasi mpya wa mgawanyiko wazuka Jubilee

Wasiwasi mpya wa mgawanyiko wazuka Jubilee

WYCLIFF KIPSANG, ONYANGO K’ONYANGO na LUCY KILALO

MATAMSHI yanayokisiwa kuwa ya mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria, yameendeleza hofu ya kuwepo kwa mgawanyiko katika chama cha Jubilee.

Bw Kuria amesikika kwa rekodi ya sauti hiyo inayosambazwa mitandaoni akidai kuwa viongozi wa Mlima Kenya wanaomuunga mkono Naibu wa Rais William Ruto wamepata vitisho.

Bw Kuria anawahakikishia wenyeji wa bonde wa ufa kwamba Mlima Kenya utamuunga mkono naibu wa rais mwaka wa 2022.

“Wengine wetu mkituona hapa tunapokea vitisho kila siku eti tunamfuata Ruto. Nilifikiria kumuunga Naibu wa Rais ni sehemu ya ajenda ya Jubilee,” Bw Kuria anasema kwa sauti hiyo katika sehemu fulani katika kaunti ya Nandi.

Kulingana na Bw Kuria, Rais Uhuru Kenyatta hajabadilisha nia yake ya kumuunga mkono naibu wa rais 2022.

“Hakuna wakati rais ametuambia sisi kama viongozi wa mlima Kenya kutomuunga mkono naibu wa rais,” alisema Bw Kuria.

Bw Kuria alisema kuwa hawapingi hatua ya kiongozi wa ODM Raila Odinga kuungana na Rais Kenyatta.

“Tunaunga mkono salamu kati ya viongozi lakini hatua hiyo isiwafaidi watu wachache,” alisema Bw Kuria.

Kumekuwa na minong’ono katika muungano wa Jubilee kufuatia madai kuwa baadhi ya viongozi wako na nia ya kuhakikisha kuwa Bw Ruto hashindi urais mwaka wa 2022.

Kiongozi wa walio wengi katika bunge la seneti Kipchumba Murkomen amethibitisha kuwa mambo si sawa katika muungano wa Jubilee.

“Tuko na habari kuwa kuna baadhi ya watu katika afisi ya rais ambao wanatumia muda wao mwingi kuhakikisha kuwa Jubilee inasambaratika,” Bw Murkomen alisema kwenye mahojiano ya moja moja katika runinga ya Citizen Jumapili usiku.

Kulingana na Bw Murkomen, wanaompiga Ruto vita ni wale hawataki yeye atwae urais mwaka wa 2022.

Wakati huo huo, Mbunge wa Cherangany, Joshua Kutuny alipuuzilia mbali kuwepo kwa mgawanyiko katika Jubilee, huku akitahadharisha wafuasi wa Naibu Rais dhidi ya kujitenga na salamu kati ya Rais Kenyatta na kiongozi wa ODM, Raila Odinga.

Bw Kutuny alisema Jumanne kuwa mrengo wa naibu una nafasi kubwa ya kunufaika kutokana na salamu hizo, lakini ukiendelea na matamshi yanayoonekana kama ya kuwagawanya Wakenya huenda ukatengwa na kutorokwa na Wakenya wengine.

Bw Kutuny alikuwa akijibu madai ya Kiongozi wa Wengi katika Seneti, ambaye ni Seneta wa Elgeyo Marakwet, Kipchumba Murkomen, kuwa vita dhidi ya ufisadi vinamlenga Naibu Rais William Ruto.

 

Angefuata taratibu 

Alisema kuwa iwapo kuna tatizo lolote, Bw Murkomen kama mmoja wa viongozi hata kwa kundi la wabunge wa eneo la Rift Valley, alikuwa na nafasi ya kuwasilisha suala hilo kwa kufuata utaratibu wa chama wa kusuluhisha masuala yake.

“Anahitaji kuonyesha tofauti ziko wapi katika chama lau sivyo ni yeye dhidi ya chama,” alisema.

“Naibu Ruto mwenyewe anatambulika na hahitaji watu kuzungumza kiholela ili kumpigia debe.

“Kwanza wakizidi kuongea kuhusu uchunguzi wa maisha wanaibua maswali mengi zaidi kushinda majibu. Nawahimiza wenzangu kutoka Rift Valley kukoma kuzungumzia masuala ya Naibu Rais na rais.

Alisema kuwa Bw Ruto ni mtu ambaye amejijenga na mwenye tajriba ya kisiasa na ana mbinu zake za kuendesha mambo yake. Pia alitaja kuwa Bw Ruto mwenyewe ametangaza kuwa atakuwa wa kwanza pamoja na rais kuchunguzwa jinsi walivyopata mali.

zao.

“Wachunge ndimi zao, wanavyozungumza ndivyo wanaweza kuzamisha azimio la Naibu Rais la kutafuta urais,” alisema akiongeza kuwa kwa sasa ni yeye Bw Ruto pekee ambaye ametangaza nia ya urais, rais Kenyatta akitarajiwa kujiuzulu.

Hata hivyo, alitaja kuwa wafuasi wake naibu rais lazima pia umtambue Bw Raila Odinga ambaye angali katika siasa.

“Tushikilie hizi salamu, huyu baba tumbembeleze, huwezi kumpiga vita na utarajie kushinda,”

Pia alisema wanaozungumzia harakati za kuzima ufisadi wajue wanamhujumu Rais na “watangaze rasmi kwamba hatuko na Uhuru tena.”

Mbunge wa Nandi Hills, Alfred Keter na mwenzake wa Moibeni Silas Tiren pia walieleza kuunga mkono juhudi za kukabiliana na ufisadi zinazoendeshwa na rais Kenyatta.

You can share this post!

Bidhaa feki huipotezea serikali Sh200 bilioni – Ripoti

Viongozi wakashifu mauaji ya polisi na utovu wa usalama...

adminleo