Na GEOFFREY ANENE
Mshikilizi wa rekodi ya Kenya kutembea kilomita 20 kwa haraka, Samuel Gathimba amenyakua medali ya shaba kwenye Riadha za Dunia za kutembea kwa haraka jijini Muscat, Oman, Jumamosi.
Gathimba, 34, ambaye anajivunia sasa kushinda medali saba za kimataifa zikiwemo tatu za Bara Afrika, amemaliza nyuma ya Wajapani Toshikazu Yamanishi na Li Maocuo walionyakua dhahabu na fedha matawalia.
Mshindi huyo wa nishani ya shaba kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola mwaka 2018 aliridhika na shaba siku moja baada ya bingwa wa dunia wa Riadha za Dunia za chipukizi Heristone Wanyonyi kumaliza matembezi ya kilomita 10 katika nafasi ya nne kwa rekodi ya kitaifa ya dakika 45:10 naye bingwa wa michezo ya Afrika 2019 Emily Ngii akakamata nafasi ya 19 kwa muda wake bora wa 1:42:39.
Kenya pia iliwakilishwa katika matembezi ya kilomita 2o upande wa wanaume na Simon Wachira na bingwa wa zamani wa Afrika kwa watembeaji wasiozidi umri wa miaka 18 Dominic Ndigiti.