• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Uhuru atoa amri miradi Kisumu ikamilike upesi

Uhuru atoa amri miradi Kisumu ikamilike upesi

Na RUSHDIE OUDIA

RAIS Uhuru Kenyatta ametoa maagizo mapya ya kukamilishwa kwa miradi ya mabilioni ya pesa katika Kaunti ya Kisumu huku zabuni za ujenzi wa barabara muhimu zikitolewa upya kwa masharti makali.

Kutangazwa upya kwa zabuni hizo kunafuatia changamoto za kupata ardhi, kuhamishwa kwa makaburi na mabadiliko ya miundo yaliyofanya gharama kuongezeka.

Wakandarasi wameagizwa kuhakikisha kwamba miradi hiyo ya thamani ya Sh2.1 bilioni imekamilika kabla ya Novemba mwaka ujao wakati jiji la Kisumu linakapotarajiwa kuandaa kongamano la kimataifa la Afri-cities.

Kamishna wa kaunti hiyo Bi Josphine Ouko akifuata amri ya rais, aliagiza mkandarasi anayejenga daraja la Mamboleo kuhakikisha barabara zitakuwa tayari kufikia Aprili mwaka ujao wakati Rais Uhuru Kenyatta na aliyekuwa waziri mkuu Raila Odinga watakapotarajiwa kufungua uwanja wa kimataifa wa michezo wa Jomo Kenyatta unaojengwa kwa gharama ya Sh1.4 bilioni.

Kulingana na meneja wa eneo hilo wa shirika la barabara kuu nchini (KeNHA), Bw Cleophas Makau Mutua, kuna sababu nyingi na changamoto zinazoweza kucheleweshwa kukamilika kwa miradi hiyo.

“Mkandarasi alisimamisha kazi Juni 4, 2019 kwa kukosa kulipwa kazi aliyokuwa amefanya na baadaye akakatiza kandarasi akibakisha asilimia 50 kukamilisha mradi wenyewe,” alisema Mutua.

Hii imesababisha zabuni ya kukamilisha sehemu iliyobakia kutangazwa upya na kukabidhiwa kampuni ya Zhongmei Engineering Group Limited. Kampuni hiyo italipwa Sh809.9 milioni.

Ilitia saini kandarasi hiyo Septemba 18, 2020 na ikaanza kazi Novemba.Mkandarasi anayejenga barabara ya kilomita 4.5 kutoka shule ya wavulana ya Kisumu hadi Mamboleo ambaye gharama yake ni Sh2.8 bilioni ambayo ilikwama Juni 4, 2019 pia ameagizwa kuikamilisha.

Barabara hiyo ilianza kujengwa Julai 11, 2016.Ilitarajiwa kukamilika Januari 10, 2018, na licha ya muda kuongezwa hadi Disemba 21, 2019, ilikwama baada ya kampuni ya Israeli ya SBI, kusitisha kazi Juni 4, 2019 na baadaye kukatiza kandarasi Septemba 27, 2019 kwa kukosa kulipwa.

Bi Ouko alikuwa akizungumza baada ya kuongoza mkutano wa kamati ya utekelezaji miradi ya maendeleo katika Kaunti ya Kisumu.

Kaunti hiyo, ambayo ni mojawapo ya ngome kuu za kisiasa za kiongozi wa ODM Raila Odinga, imekuwa ikishuhudia mabadiliko makubwa kimaendeleo katika miaka ya hivi majuzi.

Miradi ya serikali kuu imeshika kasi tangu Rais Kenyatta alipoweka muafaka wa maelewano na Bw Odinga, almarufu handisheki, mnamo Machi 2018 baada ya uchaguzi mkuu wa 2017.

Haya yamefanya baadhi ya wadadisi wa kisiasa kutaja miradi hiyo kama ‘matunda ya handisheki’.Mradi mkuu ambao ni ukarabati wa bandari ya Kisumu haujazinduliwa rasmi hadi sasa, licha ya Rais na Bw Odinga kuuzuru mara kadhaa.

Uzinduzi uliotarajiwa uliahirishwa mara nyingi bila sababu mwafaka kutolewa na wahusika.

You can share this post!

SAMMY WAWERU: Nairobi inahitaji gavana atakayeiletea hadhi...

Corona yanusuru Sh290 milioni bungeni