• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:50 AM
Mbunge amtaka Joho ajiuzulu ODM

Mbunge amtaka Joho ajiuzulu ODM

Na CHARLES LWANGA

MBUNGE muasi wa Chama cha ODM, Bw Owen Baya amemtaka Gavana wa Mombasa, Hassan Joho ajiuzulu kama Naibu Kinara wa ODM ili wasukume azma ya kuunganisha eneo la Pwani pamoja.

Kauli yake inajiri baada ya Bw Joho na mwenzake wa Kilifi, Bw Amason Kingi wiki jana kutangaza katika hafla tofauti maeneo ya Garsen na Kaloleni, wakisema kuwa wakati umefika ambapo eneo la pwani linafaa kujisimamia kisiasa na hata kumsimamisha mgombeaji wa urais.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari, Bw Baya pia alimtaka Gavana Kingi ambaye ni mwenyekiti wa Chama cha ODM kaunti ya Kilifi pamoja na wabunge wote waliomuidhinisha Bw Joho kama kinara na msemaji wa pwani atakayepeperusha bendera ya urais 2022 kujiuzulu katika viti na majukumu yao katika chama

.’Wanafaa wajiuzulu katika majukumu yao ya chama ndio tuhakikishe kuwa hawatani na wanamaanisha wanachokisema au sivyo tutajuwa ni njama ya kuvuruga mpango wa kuunda chama cha kipwani na baadaye kurudisha wapwani kwa ODM,’ alisema.

Akijieleza ni kwa nini wanafaa kujiuzulu katika nafasi zao za chama, Mbunge huyo wa Kilifi Kaskazini alisema yeye mwenyewe aliondolewa katika ODM kama Naibu katibu mpangakazi kwa ajili ya maoni yake ya kuunda chama cha kipwani.

Wakati huo huo, Bw Baya ambaye ni mmoja wa wabunge katika mrengo wa Tangatanga inayoongozwa na Naibu Rais William Ruto, alisema wanatambua mbinu za uongozi wa kinara wa ODM Raila Odinga za kutenganisha ili kutawala ambazo huenda wanapanga kutumia kurudisha eneo hilo kwa chama cha ODM katika uchaguzi mkuu ujao.

‘Lakini wakati huu hutatukoga kwa kitumia matambiko wala pesa. Tuko tayari na imara kukomboa eneo la pwani bila wewe,’ alisema.

Viongozi wengine wa mrengo wa Tangatanga ni Mbunge wa Nyali Mohamed Ali, Khatib Mwashetani (Lungalunga), Sharif Ali (Lamu East), Jones Mlolwe (Voi), Ali Wario (Bura), Benjamin Tayari (Kinango), aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar na Mbunge wa Malindi Aisha Jumwa juwa ambaye ameweka macho yake kwa chama cha Kadu-Asili atakachokitumia kugombea ugavana wa Kilifi mwaka wa 2022.

Jumamosi iliyopita katika mazishi ya aliyekuwa mbunge wa Kaloleni Gunga Mwinga, Gavana Kingi ambaye ni mwandani wa Bw Joho alisema eneo hilo lina kura takribani 3 milioni na wakati umefika eneo la pwani linafaa kujisimamia kisiasa na kuwacha kutegemea vyama ya maeneo mengine nchini.

“Kwa ajili ya haya, ninataka kuhakikishia wakazi wa pwani kuwa ifikapo Juni mwaka huu, tutakuwa na chama chetu wenyewe ambacho kitaongoza kampeni za uchaguzi,” alisema.

Wiki mbili zilizopita, wabunge wa Tangatanga walimuidhinisha gavana wa Kwale, Bw Salim Mvurya kama kinara na msemaji wao eneo la Pwani.

Lakini Jumatano iliyopita, wabunge 25 na waziri msaidizi wa usalama, Bw Hussein Dado waliambatana na Bw Joho eneo la Garsen kupigia debe Mpango wa Maridhiano (BBI), na wakamuidhinisha Bw Joho kama kinara na msemaji wao atakayeunganisha pwani.

Akizungumza katika hafya hiyo, Bw Joho alisema wakati umefika ambapo wapwani wanafaa pia nao wasikizwe na maeneo mengine ya Kenya na kufanya misimamo zao wenyewe za kisiasa.

“Wakati umefika tutafanya uamuzi wetu wa siasa, tumekuwa tukitumiwa na watu kwa manufaa yao ya kisiasa na wakati wa kuwa wafuasi wa watu wengine umepita,” alisema na kuongeza “ukiniangalia mimi Hassana Joho au kiongozi mwengine wa pwani, kwani hatutoshi kuwa rais wa Kenya? Tumekuwa tukitumiwa vibaya kisiasa lakini wakati huu mambo yamebadilika.”

Lakini Bw Baya huenda ukubadilishaji wa uamuzi wa Bw Joho kisiasa huko Garsen ni baada ya kugunduwa mrengo wa Tangatanga umekita mizizi na kusambaa eneo la pwani.

‘Ili (Bw Joho) apate umaarufu, lazima avamia njama zetu na sasa anaitisha umoja wa wapwani pamoja na mgombeaji wa urais na yeye akiidhinishwa kama mpeperushaji bendera ya pwani,’ alisema.

You can share this post!

Jeshi lamwagwa miji mikuu uchaguzi mkuu ukinukia

CHARLES WASONGA: Ni aibu sana Rais na Naibu wake wake...