• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Amina matumaini tele Kenya itapata idhini ya kuandaa Riadha za Dunia za 2025

Amina matumaini tele Kenya itapata idhini ya kuandaa Riadha za Dunia za 2025

Na CHRIS ADUNGO

WAZIRI wa Michezo, Amina Mohamed, ni mwingi wa matumaini kwamba Kenya itapata idhini ya kuwa mwenyeji wa Riadha za Dunia za 2025 baada ya Shirikisho la Riadha (AK) kuwasilisha maombi rasmi ya kuandaa mashindano hayo ya haiba kubwa.

Kenya inashindana na Nigeria, Algeria, Misri, Morocco na Afrika Kusini kuwania fursa ya kuandaa mashindano hayo miongoni mwa mataifa ya bara Afrika.

Akizungumzia mjini Eldoret alikokuwa akikagua shughuli za ujenzi na ukarabati wa uwanjani wa Kipchoge Keino, Amina alisema: “Tuna nafasi nzuri ya kupokezwa idhini ya kuwa wenyeji wa mapambano hayo hasa ikizingatiwa kwamba tuliandaa Riadha za dunia za Chupikizi wasiozidi umri wa miaka 18 kwa mafanikio makubwa mnamo 2017.”

“Hiyo ilikuwa ithibati kwamba tuna uwezo wa kuwa wenyeji wa mashindano ya hadhi kubwa katika ulingo wa riadha duniani. Mwaka huu, tutakuwa pia wenyeji wa Riadha za dunia za Chipukizi wasiozidi umri wa miaka 20 kuanzia Julai kabla ya kuandaa mashindano ya dunia ya Safari Rally. Hili ni jambo linalotupa matumaini tele,” akaongeza.

“Tuna rasilmali za kutosha zitakazowezesha washiriki wote kushindana bila tatizo, tena kwa njia salama. Juhudi hizi za AK zimeungwa mkono na serikali kupitia Wizara ya Michezo,” akasisitiza.

Kenya iliweka wazi azma ya kuwa mwenyeji wa makala ya mbio za Diamond League mnamo 2023 na Riadha za Dunia za 2025 baada ya kuandaa Riadha za Dunia za Mabara za Kip Keino Classic kwa mafanikio makubwa mnamo Oktoba 3, 2020.

Kwa kawaida, Riadha za Dunia huvutia ushiriki wa zaidi ya wanariadha 2,000 kutoka zaidi ya mataifa 200 ili kupigania medali kwenye fani 49 tofauti kwa kipindi cha siku 10.

Kwa mujibu Jackson Tuwei ambaye ni Rais wa AK, Kenya inapania kuwasilisha ombi la kuwa mwenyeji wa mashindano hayo ya kila baada ya miaka miwili kufikia Machi 1.

Kulingana na Shirikisho la Riadha Duniani (WA), mchakato wa kutafuta mwandalizi unatarajiwa kukamilika Septemba 1 kabla ya mwenyeji rasmi kufichuliwa Disemba mwaka huu.

Iwapo Kenya itapata fursa hiyo, basi itapokezwa hadi Sh8.764 bilioni zitakazotumiwa kwa ajili ya kushughulikia maandalizi ya michezo hiyo ambayo hufuatiliwa na mabilioni ya mashabiki duniani kote na kuhudhuriwa na zaidi ya wanahabari 3,000.

“Tuko tayari kupigania nafasi hiyo. Tunajizatiti kuweka sawa stakabadhi zetu kabla ya kuwasilisha ombi rasmi kabla ya siku ya makataa,” akasema Tuwei kwa kusisitiza kwamba AK inafanya hivyo kwa ushirikiano na Wizara ya Michezo.

Hata hivyo, Tuwei hakufichua iwapo mashindano hayo yataandaliwa jijini Nairobi au Mombasa ila badala yake, akakiri kuwa watapania kutumia takriban viwanja vyote vya haiba vilivyopo nchini kwa sasa.

Kulingana na masharti ya WA, upo uwezekano mkubwa wa mashindano hayo kuandaliwa jijini Nairobi ikizingatiwa uwepo wa hoteli za haiba kubwa na viwanja viwili vya hadhi ya kimataifa – MISC Kasarani na Nyayo.

“Haya ni mashindano ambayo yatatupa jukwaa la kutangaza utajiri wa vipaji vya wanariadha wa bara la Afrika kwa ujumla. Ni mashindano ambayo pia yatatuwezesha kukuza sekta ya utalii na kujivunia tamaduni za jamii mbalimbali. Afrika haijawahi kuandaa mapambano makubwa ya kiwango na hadhi hiyo,” akasema.

Kanuni za WA zinahitaji jiji linalokuwa mwenyeji wa wa Riadha za Dunia kuwa katika sehemu inayoweza kufikiwa kirahisi, uwanja ambamo mapambano hayo yatafanyika uwe na uwezo wa kubeba takriban mashabiki 30,000 walioketi na eneo la kukimbilia liwe na zulia la kisasa la kategoria 1 kwa mujibu wa viwango vya ubora wa kimataifa.

Aidha, hoteli zitakazotumiwa na vinara wa WA, wanariadha, wajumbe, washirika wa WA, wanahabari na wadau wote wengine zinatakiwa kuwa za kiwango cha kimataifa.

WA inakadiria kwamba nchi itakayoandaa Riadha za Dunia mnamo 2025 itatia kapuni mapato ya takriban Sh10.4 bilioni baada ya siku 10 za kufanyika kwa mashindano hayo.

Kenya iliandaa duru ya mwisho ya Riadha za Dunia za Mabara almaarufu Kip Keino Classic mnamo Oktoba 2020 na inatarajiwa pia kuwa mwenyeji wa Riadha za Dunia kwa chipukizi wasiozidi umri wa miaka 20 mnamo Agosti 17-22, 2021 uwanjani MISC Kasarani, Nairobi.

Barnaba Korir ambaye alikuwa mkurugenzi wa Kip Keino Classic, amesema kwamba viwango vya maandalizi vilivyoshuhudiwa katika mashindano hayo yalidhihirisha uwezo wa Kenya wa kuandaa mapambano ya haiba kubwa zaidi.

“Mbio za Kip Keino Classic zilitupa jukwaa la kujifundisha mambo mengi ambayo yatatusaidia kuwa wenyeji wa Diamond League baada ya makala mawili yajayo. Lengo letu ni kuleta mashindano hayo hapa Kenya na kudhihirishia ulimwengu ukubwa wa uwezo wetu katika kuandaa matukio makubwa hata zaidi,” akasema Korir.

Tangu yaasisiwe mnamo 2010 kuchukuwa nafasi ya mbio za IAAF Golden League, mashindano ya Diamond League ni miongoni mwa mapambano 15 ya haiba kubwa zaidi ambayo huandaliwa na Shirikisho la Riadha Duniani (WA) kila mwaka.

Mbio hizo hujumuisha fani 16 tofauti zikiwemo mbio za mita 100, mita 200, mita 400, mita 400 kuruka viunzi, mita 800, urushaji wa kijiwe, urushaji wa kisahani, urushaji wa mkuki, kuruka juu na kuruka juu kwa upande wa wanawake na wanaume.

Hadi kufikia sasa, ni jiji la Rabat, Morocco ndilo la pekee barani Afrika linalojivunia tija na fahari ya kuwahi kuandaa mbio za Diamond League mnamo Mei 2016.

Riadha za Dunia za Mabara almaarufu World Continental Tour ndiyo ya pili baada ya Diamond League inayofuata Riadha za Dunia (World Athletics Championships) kwenye orodha ya mashindano ya haiba kubwa zaidi kwenye ulingo wa mbio duniani.

Korir amefichua kwamba Kamati Andalizi ya Kip Keino Classic sasa itatalii baadhi ya mapungufu machache yaliyoshuhudiwa kwenye mbio hizo za Oktoba 3, 2020 kabla ya kubuni mikakati maridhawa zaidi itakayofanikisha maandalizi ya Diamond League mnamo 2023.

Riadha za Kip Keino Classic ndiyo mashindano ya kwanza ya haiba kubwa kuwahi kufanyika barani Afrika tangu kuzuka kwa ugonjwa wa Covid-19 uliositisha shughuli nyingi za michezo duniani kote kuanzia Machi 2020.

“Haimaanishi kwamba tutaridhika na ufanisi tulioshuhudia ugani Nyayo wakati wa kuandaliwa kwa mbio za Kip Keino. AK itazidi kushirikiana na Wizara ya Michezo kutalii uwezekano wa kupanua zaidi miundo-misingi iliyopo na kuwapa wanariadha wetu vifaa na mazingira mwafaka zaidi ya kujikuza kitaaluma,” akaongeza kinara huyo.

Licha ya changamoto tele za kifedha zilizochangiwa na janga la corona, Wakenya walitia fora katika mbio za Kip Keino Classic ambazo zilihudhuriwa na mashabiki 6,000. Mbio hizo zilivutia zaidi ya wanariadha 150 kutoka mataifa 30 tofauti.

Kati ya Wakenya waliotamba katika mbio hizo ni mabingwa wa dunia Hellen Obiri, Timothy Cheruiyot na Beatrice Chepkoech waliotawala vitengo vyao vya mita 5,000, mita 1,500 na mita 3,000 kuruka viunzi na vidimbwi vya maji mtawalia.

You can share this post!

Mkopo wa Ighalo kambini mwa Man-United watamatika rasmi

Afisa wa polisi auawa na majambazi eneo la Land Mawe